Tuesday, November 15, 2011

Kutana na MAEMBE AND THE SPIRITS; wakupe CHANJO YA RUSHWA.

Ni ukweli usiopingika kuwa,Tanzania ya sasa inagubikwa na wimbi la WANAHARAKATI wa kila aina kuanzia wa kisiasa, kiuchumi na wale wa kijamii. Kimsingi katika nyanja zote za maisha ya mwananchi wa tanzania, wanaharakati wametokea kuonesha mapambano, na mara nyingi yamekuwa ni ya kujaribu kuzirekebisha taasisi au asasi husika ambazo kwa namna moja ama nyingine zimekuwa zkionesha dalili ama moja kwa moja kuonesha kupindisha haki, kunyima demokrasia, kuzuia ukuaji wa uchumi wa nchi na maendeleo ya wananchi na matakwa ya watanzania kwa ujumla.


Maembe And The Spirits, ni miongoni mwa wanaharakati walioamua kujitosa katika msitu wenye simba wengi katika harakati za kukabiliana na tatizo sugu la RUSHWA nchini Tanzania na kwingineko duniani. Kikundi hiki, kikiongozwa na bwana Vitali Maembe, kwa kutumia nyimbo mbalimbali wanazotunga wenyewe pamoja na majadiliano ya wazi, kimeamua kwa gharama zao, kutembelea maeneo yote ya Tanzania ili kuwaelimisha watanzania mambo mbalimbali yahusuyo rushwa yakiwemo madhara, vyanzo na namna ya kuepukana na kansa hii sugu iliyomea katika damu za watu na inoyoonekana kushindwa kutibika kirahisi. Maskani yao hasa ni Bagamoyo.

Harakati yao hii wanayoiita CHANJO YA RUSHWA inayobeba ujumbe "kuiba, kutamani kuiba,kuweka mali ya wizi,kumficha mwizi, kumtamanisha mwizi ni kosa la wizi". Wanamaliza kwa kusema kuwa, "Rushwa ni Adui wa haki na maendeleo". Kwa maneno mengine, Maembe and The Spirits, wanatuambia kuwa, kula rushwa, kutamani kula rushwa,kumficha mla rushwa, kumsabibishia mtu kula rushwa ni Rushwa.

Hadi sasa wanaharakati hawa wameshatembelea katika Taasisi, wanajamii na Asasi  nyingi za hapa nchini wakitoa chanjo hii ya rushwa kwa njia ya nyimbo. Haya ni mafanikio makubwa. Kwa kuwa wanaelimisha jamii kwa njia ya njimbo, pia wanapata fursa ya kuiburudisha jamii.

Kama inavyojulikana, vita dhidi ya rushwa ina maadui wengi kwa kuwa wafuasi ni wengi wasiopenda kuingiliwa. Hivyo,mbali na mafanikio waliyokwishayapata, changamoto nazo zimekuwa ni sehemu ya harakati zao. Siandiki hili kwa utashi wangu lakini mbali na kukutana na wanaharakati hawa na wakaweza kueleza miongoni mwa changamoto wanazokabiliana nazo katika harakati zao za kuikabili rushwa, Bwana Vitali Maembe ameeleza hapa katika blogu yao waiitayo CHANJO YA RUSHWA miongoni mwa changamoto hizi wanazokabiliana nazo. Changamoto nyingine ni pamoja na nyimbo zao nyingine kutopewa nafasi katika baadhi ya vyombo vya habari na kushindwa kuzifikia baadhi ya taasisi kutokana na vikwazo wanavyokumbana navyo vinavyotokana na taasisi husika.

Hakika kazi wanayoifanya ni kubwa na ikizingatiwa kuwa wanajitolea. Tuwaunge mkono kwa kila hali katika harakati za kutokomeza kabisa Rushwa hapa nchini. Nimalizie kwa kusema kuwa, tabia inabadilika, rushwa ni tabia, hivyo tunaweza kubadili mitizamo yetu kwa kuikataa rushwa katika mazingira yote kama wasemavyo Maembe and The Spirits kuwa kuiba, kutamani kuiba,kuweka mali ya wizi,kumficha mwizi, kumtamanisha mwizi ni kosa la wizi.





Wednesday, July 27, 2011

Hii ni Sayansi au Imani?




Kuna mambo mengine katika hali ya kawaida, tunayatenda lakini kuyaelezea inakuwa vigumu. Tunatumia dawa na kusubiri kupona. Wengine wanatumia chakula na kusubiri wapate nguvu na kuona miili inajengeka. Maelezo ya nini kinatokea hadi haya yanafanyika, mara nyingi yanakuwa si muhimu.

Picha hapo juu, inaonesha gunzi likiwa limefungwa kwenye shina na mpapai. Madhumuni ya gunzi hili ni kuzuia mpapai usiwe dume kwa maana ya kutoa maua ambayo yatatoa mapapai yasiyo ya kawaida na ambayo hayatafaa kuliwa.Nami nilishawahi kutumia njia hii miaka fulani iliyopita. Ni kweli mipapai ilikuwa inabadilika; kutoka mipapai dume na kuwa mipapai yenye kutoa mapapai mazuri yenye kufaa kula. Mapapai dume huwa yanakuwa marefu isivyo kawaida na huwa hayafai kula.

Ninachojiuliza hapa ni kuwa, gunzi hili linafanyaje kazi? Labda hii ni Sayansi na pengine yapo maelezo ya kinachotokea. Au labda, hii ni imani. Kwa maana kuwa gunzi halina msaada wowote, kwamba kingine chochote kingeweza kufungwa na muhusika akaamini kuwa mpapai ule utabadilika na kuwa jike. Si haba pia kufikiri kuwa kama hii ni imani, basi hata matumizi ya gunzi ni sehemu ya imani hiyo. Kwamba imani haitafanya kazi kama gunzi halitahusishwa.
Binafsi nilishatumia njia hii na ikafanya kazi, lakini maelezo sina. Sijui kama ni Sayansi, au ni imani. Hebu tuwaachie wataalamu (kama mzee wa Mitiki) na wengine wote wenye ufahamu na mambo haya wapate kutuondolea dukuduku hili ili hatimaye tupate kujua kama hii ni Sayansi au ni Imani.

Saturday, June 25, 2011

Pengine haikuwa busara kuwafukuza; labda harakati za kutafuta haki na usawa wa binadamu.

Tanzania tunakaribia kuadhimisha miaka hamsini ya Uhuru. Lakini kwa hali duni ya kiuchumi na kisiasa ilivyo, haitamnyima raia wa kwaida kabisa kuamini kuwa uhuru hauna maana kwake. Tazama vita kati ya wananchi na wawekezaji (wakoloni wa kizungu wa karne ya leo) unavyogharimu maisha ya watanzania. Umeme umekuwa ni tatizo sugu ambalo linaweza kutatulika. Waandishi wa habari wanakosa uhuru wao wa kufanya kazi. Haishangazi sana kwa wafanyakazi wa umma kufanya kazi nusu mwaka, mwaka mzima na hadi miaka bila kulipwa stahiki zao ikiwemo mishahara yao. Huu ni utumwa. Inaashiria kuwa bado tuna haja ya kuutafuta uhuru ambao tunadhani tayari tunauogelea.
Hali ya utumwa unaoendelea Tanzania unanifanya niamini kuwa, kwa kuwafukuza wakoloni wa kizungu haikumaanisha kuwa tulipata uhuru na hivyo tukawa huru. Nadhani tulipaswa kutambua tu kuwa, waafrika asili yetu ni Afrika na ili tuwe huru hakukuwa na umuhimu wa sisi (waafrika) kuishi peke yetu(kujitenga) kama ishara ya kuwa huru. Hata hivyo jambo hili halijawezekana.

Binafsi ninaona ni bora harakati za kutafuta haki za binadamu zingepewa kipau mbele kuliko kutafuta uhuru kwa kuwafukuza wale walioonekana kuficha na kuwakosesha uhuru wazawa.

Inashangaza kidogo kwani wale tuliowafukuza katika harakati zetu za kutafuta uhuru, ndio haohao leo hii wamekuwa ndio kimbilio letu. Leo hii tunawafuata na kuwaomba waje kwetu kutusaidia kutumia rasilimali zetu; wawezeshe mipango ya muda mrefu na mfupi kwa kuwa wahisani wetu katika bajeti ya serikali. Miaka hamsini tutajivunia kuwa tumejenga barabara kwa hisani ya watu wa china, hospitali zimejengwa kwa hisani ya serikali ya Uingereza na kadhalika. Kwa mwendo huu sisiti kusema kuwa, nishati ya umeme imekuwa ni tatizo kwa kuwa hakuna wahisani!

Miaka hii hamsini sijui tunajivunia nini wakati wale tuliowafukuza ndio hao tunawarudia na kuwapigia magoti warudi kiuwekezaji. Uwekezaji katika maeneo mengi umeshagharimu maisha ya watanzania wengi. Migogoro kati ya wananchi na wawekezaji haiishi. Idadi kubwa ya wananchi wapo gerezani bila ya hatia kwa sababu ya wawekezaji kulindwa. Tunarudi kule kwenye utumwa. Tofauti na hivi sasa ni kuwa, badala ya watu kuteswa vibaya hadharani (kuna hofu ya wanaharakati wa haki za binadamu) kwa kuchapwa viboko, kufanyishwa kazi za sulubu na hata kuuawa, wanaswekwa gerezani, na mambo mengine yanaendelea chini kwa chini. Hakuna atakayebisha kuwa, vita vile vya majimaji vimerudi tena. Utaratibu wa Ngwale upo; uwekezaji unavaa sura ya maji yale ya Ngwale.

Tanzania bado tunahitaji umakini zaidi. Pengine ifikie mahali tufikirie kuwa inawezekana kujitegemea. Ifikie mahali tusipige magoti ili kupata tunachohitaji; ifike mahali tusifikirie kutembeza "kibaba" ilihali rasilimali zituwezeshazo kukijaza kibaba chetu wenyewe zipo. Na,haina maana kupewa fedha ili kukuza uchumi, ni afadhali kuwezeshwa kujipatia fedha ili kujikuzia uchumi wetu wenyewe. Tukiendelea kutembeza kibaba hasahasa kwa wale tuliowafukuza katika harakati za kudai uhuru, basi mimi, wewe na yule (pengine) hatutashindwa kufikiri kuwa, haikuwa busara kuwafukuza wakoloni, badala yake kumbe kilichotakiwa ni kuanzisha "harakati za kutafuta haki na usawa wa binadamu".

Friday, June 10, 2011

Labda B.W Botha alitumia tafsida.

P.W Botha alikuwa ni raisi wa zamani wa Afrika ya Kusini wakati nchi hii ilipokuwa inatawaliwa. Kuna wakati Raisi huyu alilihutubia baraza lake la mawaziri na nakala ya hotuba yake iliandikwa katika gazeti la Sunday times la Afrika Kusini na David G. Mailu tarehe 18 August 1985.

Botha aliongea mengi yaliyoonekana kuwakashifu waafrika. Miongoni mwa mambo aliyoyayongelea ilikuwa ni hili: "By now everyone of us has been seen it practically that Blacks cannot rule themselves. Give them guns and they will kill each other".
Naam, hadi sasa, nchi zote za Afrika hazitawaliwi tena na wakoloni wa kutokanchi za ng'ambo; tulishapata uhuru wa kujioongoza kama sio kujitawala. Hali halisi inaonesha tunashindwa kutumia vizuri ule uhuru wa kujiamulia mambo yetu wenyewe; uhuru ambao tuliutafuta wenyewe kwa kumwaga damu ilipobidi. Najaribu kutafakari kuhusu Afrika ya sasa. Hakuna dalili iliyowazi kweli kuwa waafrika hatuwezi kujiongoza (kidemokrasia)kama alivyosema ndugu Botha miaka kadhaa iliyopita pale aliposema: "By now everyone of us has been seen it practically that Blacks cannot rule themselves. Give them guns and they will kill each other"?

Kwa tafsiri ya leo, uhuru wa kujitawala umekuwa silaha mbaya sana. Tumevuka mipaka ya uhuru tulioutafuta wenyewe kwa hali na mali. Tumejitawala badala ya kujiongoza; tumerudisha matabaka ya kikoloni, watawaliwa na watawala.

Uhuru tulipewa (baada ya kuupigania). Hatua ambayo ilikuwa ya umuhimu sana.
Kwa hali ya Afrika ya sasa, naweza kusema kuwa Botha alitumia tafsida pale aliposema "give them (Africans) guns, they will kill each other". Yawezekana alimaanisha kuwa, wape waafrika uhuru, uone namna watakavyojitawala; uone namna watakavyokandamizana, uone namna watakavyoumizana na mwisho kuuana. Hawataitambua demokrasia inayowapasa: Ile ya kisiasa wala ile ya kiuchumi.

Ndiyo, tumepewa uhuru. Badala ya kujiongoza tumejitawala. Uhuru umekuwa silaha ya kukwamisha maendeleo. Uhuru umezaa wakoloni wazawa; uhuru umezaa silaha nyingi nyingine ambazo tunazitumia kuangamizana, tunazitumia kuuana kama alivyotangulia kusema ndugu Botha.

Ufisadi, rushwa, upindishaji wa sheria ziainishwazo wazi nakatiba na kugombania madaraka ya kutawala (wala si kuongoza), ni miongoni mwa silaha zilizoota mizizi baada ya uhuru (ambao mimi naona ni silaha nambari moja katika karne hii katika bara letu la Afrika) . Silaha hizi kiukweli zinatuua waafrika hususani watanzania.
Hali ya maisha inazidi kuwa ngumu kwa walio wengi. Tunanyanyasana, matabaka tayari yapo, tunauana wenyewe kwa wenyewe. Wazawa wachache wanatafuta kutawala (kuliko kuongoza) ili kujinufaisha wao. Wanatafuta maisha mazuri yenye kila watakalo. Wanajitahidi kurefusha maisha yao (wanazuia wao kutokufa) kwa kuua walio wengi. Tumeshuhudia migogoro ya kisiasa katika nchi nyingi za Afrika. Baadhi ni Zimbabwe, Kenya, Madagaska, Ivory Coast, Sudan, Somalia n.k. na sasa Tanzania ambapo hali ya kisiasa si ya kuridhisha. Mifano hai katika Tanzania ni mauaji yaliyotokea Zanzibar katika uchaugzi wa mwaka 2005, maualji ya watu wasio na hatia mkoani Arusha katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010, hata na yale ya Nyamongo mkoani Mara. Madhila yote haya yalikuja baada ya nguvu kubwa ya dola kutumika.
Mamia ya watu hadi sasa wapo jela pasi na hatia kwa sababu ya matumizi yasiyo stahiki ya madaraka.

Tunaodhani kuwa ni viongozi, hawaongozi bali wanatumia madaraka yao kuwachapa wanyonge kwa fimbo ya uhuru wao wa kugeuza sheria na kuzitumia kwa kadiri ya wawezavyo ili kutimiza matakwa yao. Ndio maana haishangazi kuona mahakama zetu za Kiafrika zinavyotoa maamuzi yasiyotegemewa na yasiyo ya kikatiba wala kitaaluma bali ni mashinikizo tu ya watawala fulani.
Tanzania yangu ndio hiyo inayoelekea kuadhimisha miaka hamsini ya uhuru wake. Ni yapi tunajivunia baada ya miaka hii hamsini? ujenzi wa barabara ama? shule za kata au? hospitali? Lakini tukumbuke kuwa wakoloni walijenga mashule na mahospitali mazuri sana, mengine hadi leo yanatumika na bado yapo imara. Labda Afrika ya Kusini isingekuwa kama ilivyo hivi sasa kama wakoloni wangeondoka miaka hamsini iliyopita.
Kwa mtazamo wangu, uhuru tuliutafuta ili tuweze kutumia uzalendo wetu kwa uhuru na kwa kiwango cha juu kabisa. Uzalendo hapa unabeba maana ya uwajibikaji wa kujituma kwa manufaa ya Taifa, jamii kwa ujumla na kwa mtu mmoja mmoja. Miaka hamsini tangu tupate uhuru.Tupo huru kutumia uzalendo wetu kuijenga nchi?
"Give Africans guns, they will kill each other", labda Botha alieleweka vibaya, ilikuwa ni tafsida tu!

Saturday, March 12, 2011

Inatosha sasa kuona, bora mimi kusema: Serikali yangu iharibuyo kioo itegemeacho kujitazamia.

Ni siku nyingine ya Jumamosi ambapo blogu yako ya Mwangaza inakuletea kipengele cha "Inatosha sasa kuona, bora mimi kusema".

Naam, wiki hii tarehe nane mwezi huu, wanawake duniani waliadhimisha siku yao almaarufu Siku ya Wanawake duniani. Hapa Tanzania, kilele cha maadhimisho hayo yalifanyika pia, kama ilivyozungumziwa hapa katika tovuti ya Startv.
Sina hakika sana kama maadhimisho haya yalifanyika kuanzia ngazi ya kijiji hadi kitaifa. Mimi katika pitapita yangu ya kimajukumu, nilikumbana na maadhimisho hayo katika shule ya msingi Tumuli iliyopo wilayani iramba mkoani Singida, pamoja na kuwa sikuwa na muda mwingi wa kufuatilia maadhimisho hayo.

Mgeni rasmi alikuwa mkuu wa Wilaya ya Iramba akiwa na msafara wake uliosheheni vigogo mbali mbali wa chini yake.
Mengi yaliongewa na kukamilishwa na kauli mbiu isemayo "Fursa sawa katika elimu,Mafunzo na Teknoloji:Njia ya wanawake kupata ajira bora" ambayo ndiyo kauli mbiu ya siku ya wanawake kwa mwaka huu. Iinigusa sana na kunifanya nitafakari kuhusu juhudi za serikali na hatma ya akina mama hawa wa miaka ijayo wanavyojaribu kuufikia ujumbe huu mzito katika mazingira magumu kama inavyoonekana pichani hapa chini.





















 mazingira yenyewe ndio haya, lengo litatimia?















Watoto hawa ni wa shule ya msingi Tumuli, shule ambayo maadhimisho haya yalifanyikia. Mkuu wa wilaya na wajumbe wake walifika shuleni hapo na kuelekea moja kwa moja kwenye chumba cha kupata kifungua kinywa(darasa ambapo masomo yalilazimika kusitishwa) na kisha kuelekea sehemu iliyotengwa kwa ajili ya tukio hilo.
Sina hakika kama mkuu wa Wilaya ama kiongozi mwingine aliwaza kutazama mazingira halisi ya kusomea ya akina mama hawa wa miaka ya kesho kutwa na kutathmini kama, na ni kwa namna gani ujumbe katika siku hii ya wanawake ungeweza kufikiwa katika mazingira magumu wanayokabiliana nayo akina mama hawa wa miaka ijayo kama ionekanavyo pichani juu.

Baada ya Sherehe, wakubwa hawa walirudi tena kwenye darasa maalumu kwa ajili ya kupata chakula cha mchana kilichoandaliwa vyema kabisa; wanafunzi nao walienda kupata chakula chao cha mchana (kama ionekanavyo pichani hapa chini wakiwa kwenye foleni na baadae wakiwa wamekaa "bwaloni" wakipata chakula cha mchana ) ambapo chakula kilikuwa ni mahindi makavu yaliyochanganywa na maharagwe na kupikwa kwa pamoja (almaarufu ngararimo/ndutu au makukuru kwa wachaga). Walituliza njaa yao huku wakiishia kula kwa harufu tu vile vinono vilivyoandaliwa kwa ajili ya wakubwa hao waliofanya masomo yao yasiende kama kawaida baada ya maadhimisho hayo kufanyikia shuleni hapo.



















 Wanafunzi wakiwa kwenye foleni kwa ajili ya kuchukua chakula.


Picha hapa chini, wanafunzi wakila chakula cha mchana (mahindi na maharage vilivyopikwa kwa pamoja)















Shule hii ni mchanganyiko, yani wanafunzi wa kike na kiume. Nimewaongelea hawa wa kike kwani siku hii iliwahusu sana na kauli mbiu ilikita kwenye elimu ambayo msingi wake ndipo hasa walipo akina mama hawa wa miaka kadhaa ijayo.

Naam, bado nikiwa nimejikita zaidi katika kuwaangalia akina mama wa ziku zijazo, serikali yangu ya Tanzania inashindwa kutambua (kwa makusudi) kuwa kutokutimiza wajibu wake katika nyanja mbalimbali za kielimu, kijamii na kiuchumi ni kikwazo namba moja cha kukwamisha ufikiwaji wa kauli mbiu kama hizi za siku ya Wanawake duniani(sina hakika hata kama huwa wanakumbuka kutoa tathmini ya kauli mbiu iliyopita; imefanikiwa ama haijafanikiwa na kwa kiwango gani)

Ni serikali hii hii inayoruhusu msongamano mkubwa wa wanafunzi madarasani ambapo matokeo yake ni mwalimu mmoja kuwahudumia wanafunzi wengi kuliko uwezo. Hapa bado akinamama wa kesho wanazidi kukandamizwa(akina baba wa kesho hali kadhalika) tazama darasa hili pichani. Ni chuo cha ualimu Kinampanda kilicho na uwezo wa kuchukua wanafunzi 240 tu lakini kwa sasa kina wanafunzi 577. Labda niiulize serikali katika hali hii, kauli mbiu kama hii ya mwaka huu ya wanawake itafikiwa kweli? Serekali itakwepa kulamumiwa kuwa yenyewe ndio inaongoza katika kuisaliti kauli hii ilihali haipitwi na maadhimisho haya kila mwaka na yenye kufana? Hapa sio kwamba serekali inavunjavunja kioo inachokitegemea kujitazamia?



Akina mama hawa wa leo na kesho (wapo pia akina baba wa leo na kesho) wasomao katika chuo hiki ambao nao wanatazamiwa kwenda kuwafundisha akina mama wa miaka ijayo wanatendewa haki kweli? Haitoshi, mazingira ya Wakufunzi bado nayo ni duni. Wakufunzi wapya katika chuo hiki hata na vyuo vingine kama hiki, mambo ni haya haya. Mwezi wa pili huu wanasota chuoni; hakuna hela ya kujikimu wala mishahara. Hapo hapo serekali inategemea Mkufunzi huyu atimize wajibu wake wa kutoa elimu bora ipasavyo! Jambo ambalo kwa kiasi kikubwa haliwezekani. Ndivyo serikali yangu inavyozidi kujipoteza katika harakati za kujitafuta na kama jinsi inavyozidi kuvunja kioo inachokitegemea sana katika kujiangalia taswira ya uso wake.
Tukutane tena wakati mwingine (jumamosi ijayo) katika safu hii. Jumamosi njema, mwisho na mwanzo mwema wa juma kwenu nyote. Hadi wakati mwingine, mara nyingine.

Saturday, March 5, 2011

Inatosha sasa kuona, bora kusema (Serikali ya Tanzania na usaliti kwa walipa kodi wake)

Kadiri siku zinavyoenda, nazidi kujionea namna ambavyo serikali yangu ya Tanzania inavyoonesha udhaifu mkubwa katika masuala mengi ya utendaji wake. Katika pita pita zangu, nilikutana na jengo moja lililopo katika kijiji cha Kyalosangi kilichopo wilaya ya Iramba katika tarafa ya Kinampanda mkoani Singida. Nililisogelea karibu na kisha nilikiona kibao kama kinavyoonekana hapa chini  katika picha ambacho kilinitambulisha kuwa ni mahakama ya mwanzo. Nilistaajabu maana jengo hili linaonenaka kama ni gofu na ni mda mrefu sana umepita bila kutumika. Nilfanikiwa kuomgea na mkazi mmoja na alinieleza kuwa mahakama hii inatumika na kwa bahati nzuri nami siku moja nilishuhudia watu wakipata huduma mbalimbali katika mahakama hii iliyo katika hali ya kusikitisha kwa namna jengo hili lilivyochakaa kana kwamba haina uangalizi wa aina yoyote wa wananchi na serikali .


Hiki ni kibao kinachoelekeza mahali ilipo Mahakama ya Mwanzo, Kinampanda wilayani Iramba katika Mkoa wa Singida.

 Picha hapa juu ni mwonekano wa Mahakama hii. Bado inatumika kwa shughuli za kimahakama pamoja na kuwa inanonekana kama jengo lililotelekezwa miaka mingi iliyopita.

                   Picha hapa chini zaonesha sehemu ya ndani ya mahakama hii.


                   Sehemu ya kukaa watu katika harakati za kupata huduma mbalimbali mahakamani                                                                                     hapo

Ni dhahiri kuwa watendaji na wasimamizi wa mahakama ni wazembe. Hili halina mjadala. Ni aibu kubwa kwa Serikali yangu ya jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ni aibu kwa mahakama kuonekana  kama Gofu na ilihali babo inatumika.

Pengine labda serikali inasubiri jengo hili lianguke kabisa na pengine kusababisha hata maafa (kwani siku moja laweza kuwaangukia watu wakiwa mahakamani) kisha waseme imeshatokea na hakuna namna nyingine zaidi ya kufidia wahanga (kauli kama hizi zimeshazoeleka sana na tumezishuhudia kwenye matukio mengi yakiwemo ya milipuko ya mabomu Mbagala na Gongo la mboto) na kuanza mchakato wa kujenga jengo jingine (au kutojengwa kabisa)la mahakama kwa gharama kubwa ambazo zingeepukika kwa kukarabati jengo lililokuwepo kwa kiwango kizuri na kwa gharama nafuu.

Fedha za walipakodi badala ya kuelekezwa kwenye majukumu kama haya ya kuboresha huduma za jamii, inaelekezwa sehemu nyingine ambazo hazina umuhimu kwa wakati huo (wabunge kupewa pesa kwa ajili ya kununulia magari yao binafsi ni mfano ulio hai).

Watumia mahakama hii (wananchi), labda kwa kutokujua ama akili zao kufungwa na mazoea, hili hawajaliona kama ni tatizo. Labda bado wapo kwenye ule utaratibu wa bora maisha kuliko maisha bora, au wale wa kushukuru siku imepita na bila hata kutathimini imepitaje, ama wale wa bora nimekula hata kama ni ugali wa chumvi. Jamii ya mawazo haya bado ipo miongoni mwetu na haina budi kupitwa na watati.

Huu ni uteandaji mbovu kabisa wa serikali yetu ya Tanzania, yaonesha kiwango kisichoridhisha kabisa cha utendaji. serikali isisubiri wananchi wawe wazalendo maana yanayotokea Misri na kwingineko hayataepukika. Wananchi nasi hatuna budi kufungua midomo yetu, hatuna budi kuonesha kutoridhika na huduma duni katika sehemu husika.

Friday, March 4, 2011

Inatosha sasa kuona, bora kusema-Kipengele kipya

Mwanamuzki wa kizazi kipya ndugu Joseph Haule anayejulikana sana kwa jina la Prof J aliwahi kuimba wimbo uitwao INATOSHA SASA aliomshirikisha mwanamuziki wa siku nyingi Joseph Mbilinyi almaarufu kama Mr Sugu ambaye kwa sasa ni Mbunge wa Mbeya Mjini. Prof J kuna sehemu anasema "inatosha sasa kuona nadhani bora mimi kusema" Prof J anaonesha kukerwa na mambo ambayo hayampendezi yeye, na pia yasiyoipendeza jamii vilevile. Mwanafasihi huyu anatukumbusha kuwa ifike mahali sasa tusiishie tu kuona uovu, bali na tuusemee kwa usahihi wake kwani pia ni hatua nzuri katika kutatua au kuuondoa uovu huo. Dhana hii pia si vibaya ikitumika hata kwenye mazuri katika jamii katika harakati za kuwapa moyo wale wote wenye kutenda kwa kadiri ya inavyotakiwa.


Umefika sasa wakati hata wanajamii wote, mmojammoja na hata kwa umoja wetu, tusiishie kuona tu, umefika muda wa kusema wazi kuwa haturiridhiki na huduma, haturidhiki na utendaji. Pia hatuna budi kusema pale tunaporidhika; lakini kikubwa hapa ni kuwa, imetosha kuona na sasa tuseme. Kwa mantiki hii, hata blogu ya Mwangaza nayo inaunganba na Prof J pamoja na wanajamii wote wapenda maendeleo kusema kuwa,  "Inatosha sasa kuona, bora kusema" ambacho kitakuwa ni kipengele kitakachokujia kila siku ya Jumamosi katika blogu hii ya Mwangaza. Kipengele hiki kitakuwa kinaelezea mambo mengi ambayo kwa namna moja ama nyingine yamekuwa yakifumbiwa macho na wahusika, na pia yale ambayo kwa namna moja ama nyingine, waathirika wa hali hizi ( kwa sababu mbalimbali) wameshindwa kuyaweka bayana. Vile vile pongezi hazitaachwa nyuma kwa yale mazuri yatendekayo na kwa wanaostahili. Pia kipengele hiki hakitamuacha yeyote yule atakayetaka kuonesha kuwa, naye kwa namna moja ama nyingine amechoka kuona na sasa ameona kuwa umefika wakati wa yeye kusema. Nawakaribisha sana katika kipengele hiki wadau wote wa blogu ya Mwangaza na wadau wa blogu kwa ujumla.