Kujifunza Kujifunza ni Stadi Mama ya Stadi Zote
Picha kutoka tovuti ya campaignforlearning
Tamko na 3.1.3 la Sera ya Elimu na Mafunzo, 2014
linaweka bayana kuwa elimu ya msingi ni ya lazima na inaishia kidato cha Nne. Tamko
3.1.5 linasisitiza pia kuwa, elimu hii katika mfumo wa umma itatolewa bure.
Hizi ni nia njema kabisa na za kupongezwa. Si haba kuwa, hadi sasa utekelezaji
wake unafanyika. Hata kama ni kwa taratibu au usio wa kiwango cha kuridhisha.
Swali (pengine
la msingi) la kujiuliza ni kuwa, elimu hii ya msingi inatoa msingi kweli kweli
na je Sera inaeleza bayana msingi unaopaswa kutolewa?
Sera inaweka
bayana matarajio ya ubora wa elimu na mafunzo kuanzia elimu ya awali hadi chuo
kikuu. Kwamba, elimu na mafunzo yatakayotolewa yawe ni ya “viwango vya ubora unaotambulika kikanda na kimataifa na kukidhi
mahitaji ya maendeleo ya Taifa” (uk 24).
Mwanafunzi kutoka
katika elimu yenye viwango na ubora unaozungumzwa hapo juu awe na sifa zipi?
Sera ya Elimu na Mafunzo, 2014 imeweka bayana kabisa matarajio haya. Tamko namba
3.2.5 linasema, ninanukuu:
Serikali, kwa kushirikiana na wadau, itahakikisha mitaala
inazingatia stadi za msingi za mawasiliano, kusoma, kuandika na kuhesabu;
kutafiti; kuchambua taarifa; kutafsiri, kutathmini na kutumia maarifa, uvumbuzi,
ubunifu na ujasiriamali katika ngazi zote za elimu na mafunzo.
Kwamba, kwa
vyovyote vile, mwanafunzi anayepitia kwenye mfumo wa elimu wa Tanzania
anatarajiwa kuwa na uwezo wa kuwasiliana vyema, kuwa mbunifu, mtafiti,
mchambuzi makini wa taarifa, uvumbuzi n.k. Kwa hakika, soko la ajira linahitaji
watu wa namna hii. Iwe kwa kujiajiri ama kuajiriwa.
Ukiacha
stadi za kuhesabu, kusoma na kuandika, hizi stadi nyingine zinafundishwa wapi
au ni wapi zinajitokeza wakati wa kujifunza? Kupitia Sera ya elimu na Mafunzo,
Serikali imeweka lengo la kuwa na mazingira bora ya kufundishia na kujifunzia. Katika
lengo hili, tamko namba 3.2.9, linasema, ninanukuu;
Serikali itahakikisha vifaa,
nyenzo na zana stahiki za kufundishia na kujifunzia katika elimu na mafunzo zinatosheleza
kulingana na mahitaji na maendeleo ya sayansi, teknolojia na mbinu za
kufundishia na kujifunzia katika ngazi zote.
Hata hivyo,
tusisahau msemo wa wahenga, kuwa, penye miti mingi hapana wajenzi. Mazingira ya
ujifunzaji na ufundishaji yanaweza kuwa bora kabisa lakini matarajio ya viwango
wa vya ubora wa elimu unaotarajiwa yasionekane. Tunao wasimamizi wa elimu
wanaoweza kutafsiri kwa ufasaha matakwa ya miongozo ya elimu ikiwamo sera hii?
Kwa mfano, ni walimu wangapi wanachukua muda wao kusoma Sera ya Elimu wanayoitekeleza?
Ikiwa
ubunifu, uchambuzi wa kina wa taarifa, utafiti, uvumbuzi si msomo ya moja kwa
moja kwenye mitaala hususani kwenye elimu ya msingi, wanafunzi wanazipatia wapi
stadi hizi muhimu katika karne hii na karne zinazokuja? Walimu wanazifahamu na
kutambua umuhimu wa stadi hizi kwenye soko la ajira?
Kimsingi,
bado tunakosa stadi ya msingi sana ambayo ni mama wa stadi zilizoainishwa
kwenye sera ya elimu na mafunzo. Kujifunza kujifunza au kwa lugha rahisi
kujifunza namna ya kujifunza. Ukosefu wa stadi hii ni donda sugu linalotumaliza
watanzania kuanzia ngazi ya viongozi wakuu na kila mmoja wetu.
Kujifunza
namna ya kujifunza kunamfanya mtu kuwa na tabia ya ujifunzaji endelevu (lifelong
learning). Hakuna kitu ambacho maisha yote kitaendelea kuwa kama kilivyo.
Kwamba, ukishakijifunza, ndio kitaendelea kuwa hivyo milele. Kukumbatia hali
hii kunatufanya kuwa watu wa kufanya mambo kwa mazoea na hivyo kuzuia
mabadiliko chanya hata mazingira yakiwa rafiki kwa kiasi gani.
Stadi ya
kujifunza kujifunza kama nilivyodokeza awali, inamfanya mtu kuwa mjifunzaji
mwendelevu. Bila kuwa na tabia ya ujifunzaji endelevu, si rahisi kuwa mbunifu,
mtafiti, mchambuzi wa kina, na mvumbuzi. Tatizo hili linatuathiri vibaya sana
kwenye utendaji wetu wa kila siku kwa namna mbalimbali.
Kuwa na
kipaji haimaanishi kuwa itafika mahali bila juhudi yoyote utaweza kukitambua na
kukifanyia kazi. Inahitajika juhudi ya kukitambua, kukifanyia kazi na
kukiendeleza. Kuhitimu masomo, haimaanishi kuwa yale uliyojifunza shuleni,
utayakuta kama yalivyo kazini.
Katika
mazingira kama haya, kuna jambo la ziada linahitajika. Kwanza, kuwa na stadi ya
kujifunza kujifunza. Stadi hii inatoa fursa ya kuwa tayari kujifunza kulingana
na mazingira. Hii inakaribisha ubunifu, uvumbuzi, utafiti, kufikiri kwa kina
alimradi kukabiliana na changamoto. Huku ndiko kujifunza kunakohitaji uwezo wa
kujua namna ya kujifunza.
Tukihitaji
ufanisi wa vijana wa umri chini ya miaka 17 kwenye mpira wa miguu kwa mfano,
haitoshi tu kuwatumia kwa kuwa wana vipaji. Wanahitaji elimu inayoelezwa kwenye
sera ya elimu na mafunzo, 2014. Wanahitaji ubunifu, tafakari pana, uvumbuzi,
n.k. Mambo ambayo ikiwa hawana ujuzi/ stadi ya kuwa tayari kujifunza na
kujifunza namna ya kujifunza, hatutokaa kuona mafanikio ya kusonga mbele
yanayotarajiwa kutoka kwako. Itakuwa kawaida tu nap engine ule msemo wa kichwa
cha mwendawazimu utaendelea kushamiri.
Elimu ya
msingi ni kila kitu, hivyo iwe ya msingi kwelikweli. Ni muhimu kuelewa misingi mikuu inayopaswa kuwekwa ni ipi. Ubunifu, uwezo wa kuwasiliana, uvumbuzi, utafiti, uchambuzi, utumiaji wa maarifa n.k ni miongozi mwa mambo yanayotarajiwa kwenye elimu yetu msingi.
Juu ya yote, stadi ya
kujifunza namna ya kujifunza ni mama wa stadi zote. Ni moja ya misingi muhimu wanayopaswa kujengewa watoto na wanafunzi wetu. Ujifunzaji endelevu ni
matokeo ya stadi na ujuzi wa kujifunza kujifunza. Msingi huu utawasaidia wanafunzi katika ngazi za elimu zinazofuta na hivyo kuwaandaa kuwa wanafunzi endelevu, kuwa na ufanisi kazini, kuweza kujiari na hatimaye kuleta tija kwenye jamii, kitaifa na kimataifa.
Comments