Elimu inayozingatia uwezo(Competence Based Education): Maana na Misingi yake Mikuu



Matumizi ya TEHAMA ni moja ya njenzo muhimu ya kufanikisha Elimu inayozingatia uwezo mashuleni. Kupitia TEHAMA, wanafunzi wanaweza kujisomea popote na kwa wakati wao huku wakishirikiana na wenzao popote pale walipo. Picha kutoka HakiElimu


Kama nilivyotangulia kuandika katika makala iliyotangualia, ni takribani miaka kumi na ushei tangu elimu inayozingatia uwezo ilipoanza kutumika rasmi nchini Tanzania. Katika kipindi hiki, hakujakuwa na mafanikio ya kuridhisha sana katika ngazi zote za elimu. 

Wanafunzi wengi wanamaliza elimu ya msingi bila kujua kusoma wala kuandika, wanafunzi wengi wanamaliza shule za sekondari wakiwa wamepata madara yasiyoridhisha. Vile vile, vijana wa vyuo vikuu wanamaliza vyuo bila kuwa na stadi stahiki za kukabiliana na changamoto za kukosekana kwa ajira n.k.

Elimu inayozingatia uwezo ilitazamiwa kuwa ingeweza kukabiliana vyema na changamoto hizi za kufeli kwa wanafunzi pamoja na suala la ajira hususani kwa vijana wanaomaliza vyuo vikuu. Lakini, swali la kujiuliza ni kuwa, mfumo huu wa elimu kwa takribani miaka kumi ya uwepo wake, umetendewa haki au tuishie kusema kuwa siyo muafaka kwa mazingira yetu? Walimu wanaufahamu wa kutosha wa elimu hii? Je, ni kweli fikra za walimu na wanafunzi katika ufundishaji na ujifunzaji zinaongozwa na misingi ya mfumo huu? 

Tafiti mbalimbali zilizoangalia matumizi sahihi ya elimu inayozingatia uwezo zinaonesha kuwa mfumo huu bado haujatumika ipasavyo mashuleni na hata vyuoni. Mambo kadhaa yameoneshwa kuwa yanahitajika kufanyiwa kazi. Suala la kwanza ni elimu kuhusu mfumo huu wa ufundishaji na ujifunzaji. Suala la pili ni uboreshaji wa mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji. Lengo la Makala haya ni kujaribu kutatua changamoto ya kwanza, hii ya ufahamu kuhusu elimu inayozingatia uwezo. Nitajadili kuhusu maana pana ya elimu hii na misingi yake mikuu mitatu. 

Elimu inayozingatia Uwezo (Competency Based Education) ni nini?
Elimu Inayozingatia Uwezo ni mfumo wa elimu usiozingatia muda ambao mwanafunzi anapaswa kuutumia kujifunza kama kigezo cha kuwa amehitimu masomo bali hujikita kwenye maendeleo ya mwanafunzi kitaaluma kwa kuangalia kama mwanafunzi husika amefikia malengo ya ujifunzaji yaliyokusudiwa au bado hajayafikia. 

Hii ina maana kwamba, muda siyo kigezo cha kumfanya mwanafunzi ahame ngazi moja ya elimu kwenda nyingine au kuhama mada moja kwenda nyingine. Kigezo kikubwa ni kama mwanafunzi amefikia lengo la kujifunza lililokusudiwa. Kama bado, ataendelea kujifunza hadi atakapofanikiwa. 

Kwa mfano, wanafunzi wanaojifunza kusoma na kuandika darasa la kwanza, hawataondoka darasa hilo hadi watakapoweza kusoma na kuandika, hata wakijifunza kwa zaidi ya mwaka mmoja. Wale wanaoweza kusoma na kuandika, wataendelea na ngazi nyingine, hata kama mwaka haujaisha. Huu ndio mfumo wa elimu inayozingatia uwezo kuliko umri au muda alioutumia mwanafunzi kujifunza. 

Bahati mbaya, walimu wengi mbali na kuwa dhana hii bado ni ngeni kwao, lakini pia, ni dhahiri kuwa, kwa mfumo maarufu wa kusoma kwa kuzingatia muda, utekelezaji wa mfumo huu bado una changamoto kubwa ya kuweza kutekelezwa ipasavyo hapa Tanzania. 

Mfumo huu wa elimu una misingi mikuu mitatu. Msingi wa kwanza ni kuwa, mwanafunzi ndiye kiini cha ujifunzaji (Learner-Centric)

Katika msingi huu, ujifunzaji unamlenga mwanafunzi mmoja mmoja (learner-centric). Mwanafunzi anapewa fursa ya kujifunza kwa wakati wake, popote alipo na wakati huo akishirikiana na wenzake kwenye kufikia malengo yake ya ujifunzaji. Mwanafunzi mmoja akifikia malengo yake ya ujifunzaji, haimaanishi kuwa ni lazima kwa wakati huo, wanafunzi wengine wanapaswa pia wawe wamefikia malengo ya ujifunzaji yaliyokusudiwa. Kila mwanafunzi hujifunza kwa wakati wake kulingana na uwezo wake. 

Msingi wa pili wa elimu inayozingatia Uwezo ni ujifunzaji unaozingatia matokeo (Outcome Based). 

Hii ni aina ya ujifunzaji ambayo hujikita zaidi kwenye kuhakikisha mwanafunzi amefanikiwa kupata kile kilichokusudiwa kwenye kujifunza. Siyo kuwa mwanafunzi ameelewa kwa kiasi gani, bali ameelewa au hajaelewa, amefikia lengo au hajafikia lengo. Mwanafunzi hataruhusiwa kuendelea na ngazi nyingine hadi pale kutakapokuwa na ushahidi usio wa mashaka kuwa, alichopaswa kujifunza amekielewa kwa kuzingatia vigezo vilivyowekwa. 

Kwa hiyo, katika mfumo huu, jambo la kwanza kabisa linaloshauriwa ni kuhakikisha malengo mahsusi ya ujifunzaji yanaainishwa kwa ufahasaha na kwa umakini. Pia, kuhakikisha kuwa kuna vigezo madhubuti vya kuonesha kama mwanafunzi amefikia malengo au bado hajayafikia. Hii ni pamoja na kuwa na njia muafaka za upimaji na utoaji wa tathmini ya ufikiwaji wa malengo yaliyokusudiwa kwa wanafunzi. 

Msingi wa tatu wa elimu inayozingatia uwezo ni ujifunzaji unaozingatia mahitaji maalum ya mwanafunzi (Customized Learning). 

Misingi huu una maana kuwa, kila mwanafunzi ana mahitaji yake ya msingi ili kujifunza kwa tija. Wanafunzi wanatofautiana mitazamo, uwezo wa kiakili, uwezo wa wazazi kifedha na hata tamaduni. Kwa hiyo, mazingira ya ujifunzaji ya mwanafunzi mmoja mmoja ni lazima yaboreshwe na kubadilishwa ili yaendane na mahitaji ya mwanafunzi husika (customized learning). Nyezo za kujifunzia, mbinu na mazingira yanapaswa kuendana na matakwa ya mwanafunzi mwenyewe. Hata kile anachopaswa kukisoma, kinapaswa kiendane na matarajio, malengo na machaguo ya mwanafunzi mwenyewe. 

Ukweli ni kuwa, misingi hii ya elimu inayozingatia uwezo bado ni migumu sana kuitekeleza katika mazingira ya Tanzania. Angalao msingi mmoja tu wa mwanafunzi kuwa kiini cha ujifunzaji ndio unaotekelezwa. Hata hivyo, ni kwa kiasi kidogo sana.

Ili kufikia vyema malengo ya kumfanya mwanafunzi kuwa kiini cha ujifunzaji wake, moja ya nyenzo muhimu sana ni matumizi ya TEHAMA kwenye ufundishaji na ujifunzaji. Tanzania bado tupo nyuma sana. Vitabu havitoshelezi, shule nyingi hazina miundombinu rafiki kama ya umeme na kadhalika. Hali hii bado inapelekea wanafunzi kutumia fursa chache zinazopatikana mahali Fulani tu kuhakikisha wanajifunza, muda wa kuhitimu ukifika, wote watahitimu, walioshindwa kufika malengo yao na wale waliofikia malengo yao ya kujifunza. Na hapa, dahana ya usawa katika kujifunza inakuwa imepotea.

Hata hivyo, hadi sasa, kuna juhudi kubwa nchini Tanzania zimeshafanyika na zinazoendelea kufanyika kuhakikisha wanafunzi wanafikiwa walipo katika kupata elimu kupitia TEHAMA. Baadhi ya makampuni binafsi na taasisi za serikali kama vile Ubongo Kids,  Edmodo (Chuo Kiuu cha Dodoma), elimu popote (Uhuru One) na wengine wengi wameshafanya kazi nzuri ya kuhakikisha elimu inapatika popote alipo anayependa kujifunza.

Comments

Albert Kissima said…
Asante Anna, karibu hapa kibarazani kwangu.

Popular posts from this blog

Mambo Makuu Manne ya Kuzingatia ili Kufanya Upimaji Endelevu Wenye Tija

Mambo Muhimu ya Kuzingatia Katika Kuboresha na Kuongeza Ufanisi wa Shule.

Kubadilika kwa Mitaala: Walimu na Wanafunzi Wabadilike kwa Namna Gani?