Shairi: Kilio cha Albino



                   Picha kutoka Yahoo news

Kisa ni mbovu imani, Ndugu zetu mwawaua, [ Amir Kulanteni]
Mwamuabudu shetani, Mmezitupa sheria,
Twapita tu duniani, Kifo chaja kwenu pia,
Kilio cha Albino, Hivi kweli tunajali?

Wenye dhima mwafanyani? Uhai kutulindia,
Wananchi mashakani, Nyie kiguu na njia,
Mara mpo marekani, Sisi huku tunalia,
Kilio cha Albino, Hivi kweli tunajali?

Mwaiba mabilioni, Mwashindwa kututetea,
Ni kama watu usoni, Moyoni mwatumendea,
Ni kama tu hayawani, Imani zimepotea,
Kilio cha Albino, Hivi kweli tunajali?

Vitendo vyangoja nini?, Matamko tu mwatoa,
Ndugu zetu kaburini, Hamuioni kadhia,
Matendo ya kishetani, Nyie mwayakaushia,
Kilio cha Albino, Hivi kweli tunajali?

Twendeni makanisani, Tuombe huku twalia,
Twendeni misikitini, Tuzisome kali dua,
Mungu na awalaani, Motoni aje watia,
Kilio cha Albino, Hivi kweli tunajali?  

Amiri wa Kulanteni, Beti umezipatia,       [Mutabazi Muta Mutabe]
Ujumbe zimesheheni, Saluti nakupigia,
Ni qadar ya manani, Si hali walonunua,
Kilio cha Albino, Sioni kama twajali.

Tungeingia vitani, Madhubuti pigania,
Twaishia viririni, Badae twapuuzia,
Mungu tumjibu nini, Siku ikishawadia,
Kilio cha Albino, Sioni kama twajali.

Twakomaa vijiweni, Mpira kuongelea,
Twaingia huzunini, Mechi tukijikosea,
Albino mdomoni, Moyoni twajipetea,
Kilio cha Albino, Sioni kama twajali.

Siishie facebukuni, Makali kuoneshea,
Tuingie mitaani, Watu kuhamasishia,
Aridhia Rahmani, Haki tukipigania,
Kilio cha Albino, Sioni kama twajali.

Simanzi tele moyoni, Binadamu kuuana,     [Albert Kissima]
Tumekuwa hayawani, Rabuka tumemkana,
Utu u wapi jamani, Tunusuru maulana,
Kilio cha Albino, Hivi kweli tunajali?

Ni ajabu duniani, Ugonjwa kuwa ni dili,
Kisa hii melanini, Binadamu kawa mali,
Potofu hii imani, Tupinge kwa kila hali,
Kilio cha Albino, Hivi kweli tunajali?

Kwa panga wanawakata, Albino wakiwa hai,
Mateso wanayopata, Nani ambaye halii?,
Dhoruba itawakuta, Kamwe habaki adui,
Kilio cha Albino, Hivi kweli tunajali?

Viungo vya binadamu, Kutolewa akiwa hai,
Kwa mapanga sina hamu, Kuvumilia haifai,
Na kamwe hayatadumu, Wauaji mabedui,
Kilio cha Albino, Hivi kweli tunajali?

Hali hii hadi lini, Tunaweza kukabili,
Kwa pamoja tulaani, Sote na tuwe wakali,
Tuwaweke hadharani, Wauaji mafedhuli,
Kilio cha Albino, Hivi kweli tunajali?

Baraka wa Cosimasi, Albino wa Sumbawanga,
Mungu akupe wepesi, Na azidi kukuchunga,
Upone kwa kasi, Akulinde na majanga,
Kilio cha Albino, Hivi kweli tunajali?

Ulale pema Yohana, Alubino wa Geita,
Hakupenda Maulana, Madhila yalokukuta,
Tunamuomba rabana, Wengine kutowakuta,
Kilio cha Albino, Hivi kweli tunajali?

Dola chukua hatua, Madhila kuyamaliza,
Raia tukiamua, Kukomesha tunaweza,
Ndugu zetu wanalia, Ni sharti kuwatuliza,
Kilio cha Albino, Hivi kweli tunajali?          

Shairi hili limeandaliwa na Amir, Ashiru na Albert.

Comments

Amos Msengi said…
Nadhani kunayo haja ya kutubu mbele za Mungu maana tumekosea sana kuwafanya ndugu zetu albino waone dunia kama sio kwao, sizani kama ni accident kwao kuzaliwa katika dunia hii.

Mungu tusamehe wote.
Amos Msengi said…
Kisima mambo yako vipi? Uko bize Siku hizi ndio kusema kitabu kimebana sana?

Nakusalimu sana.

Popular posts from this blog

Mambo Makuu Manne ya Kuzingatia ili Kufanya Upimaji Endelevu Wenye Tija

Mambo Muhimu ya Kuzingatia Katika Kuboresha na Kuongeza Ufanisi wa Shule.

Kubadilika kwa Mitaala: Walimu na Wanafunzi Wabadilike kwa Namna Gani?