Namna Walimu Wanavyoweza Kuboresha Ufundishaji Kwa Kutumia TEHAMA



                                                      
                         Picha ya sehemu ya ndani ya moyo kutoka kwenye moja ya Video inayoelezea    mfumo wa mzunguko wa damu
Kwa kipindi cha miaka ya 2011 hadi 2013 nilikuwa mmoja wa wawezeshaji wa mradi wa kuwawezesha walimu wa shule za sekondari kutumia Teknologia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kwenye mchakato wa ufundishaji na ujifunzaji. Mradi huu ujulikanao kama SME (Science, Maths and English)-ICT Project, ulikuwa unatekelewa na Wizara ya Elimu na mafunzo ya Ufundi (MoEVT).
Mradi huu ulilenga masomo ya sayansi ambayo ni Biolojia, Kemia na Fizikia. Masomo mengine yalikuwa ni Kiingereza na hisabati. Kwa mujibu wa tafiti, masomo haya yalionekana wanafunzi wanafeli sana, na hivyo moja ya namna ya kukabiliana na changamoto hii ilikuwa ni kuanzishwa kwa mradi huu wa majaribio.
Walimu walifundishwa namna ambavyo wangeweza kutumia kompyuta pamoja na vifaa vingine kama projekta kwenye ufundishaji na ufunzaji. Lengo kuu lilikuwa ni kutumia TEHAMA katika kurahisisha ufundishaji wa dhana ngumu ambazo hata pamoja na ufafanuzi wa mwalimu, dhana hizi bado zisingaliweza kueleweka kwa wanafunzi. Mfano, katika somo la biolojia, mada kama za mifumo ya mmeng’enyo wa chakula, mfumo wa damu, utoaji taka n.k mwalimu anaweza kupata shida kufundisha kinadharia, lakini kwa msaada wa TEHAMA, wanafunzi wanaweza kutazama video au animation zinazoonesha mfano wa mchakato halisi.
Mradi huu ulihusisha walimu wachache. Hivyo, lengo la Makala haya ni kumuelekeza mwalimu namna anavyoweza kupata zana za kidigitali za kufundishia na kujifunzia na namna anavyoweza kuzitumia.
Kwa bahati nzuri, wakati wa mradi, ilifanyika juhudi kubwa ya kupata zana za kidigitali za kufundishia na kujifunzia kwa masomo ya sayansi, kiingereza na Hisabati. Kupia Wiki ya mradi, unaweza kupakua baadhi ya zana hizi za fizikia hapa (kama zinaendana na somo unaloliandaa) au ukafuata link ulizopewa hapa zinazokupeleka kwenye zana za masomo tofauti kulingana na uhitaji wako.
Zana hizi za kidigitali za kufundishia na kujifunzia zinaweza kuwa ni video, animation, sauti  na picha, bila kusahau na maandishi kama vile vitabu na majarida. Kwa animation, ili ifunguke, inashauriwa kwenye kompyuta yako/ simu uwe na vitumizi  kama  vile Java na adobe flash player. Unaweza kuipakua java hapa na dobe flash player hapa.

Moja ya tovuti nzuri sana zenye mkusanyiko wa zana za kidigitali za kufundishia na kujifunzia ni PHET. Hadi sasa, tovuti hii ina zaidi ya simulations milioni 200 za masomo ya Kemia, Fizikia, Biolojia, Hisabati n.k. Shukrani kwa timu ya PHET kwani zana hizi ni bure kabisa. Mwalimu, mwanafunzi au mwingine yeyote hana haja ya kuzinunua. Ila, unaweza kuchangia kama sehemu ya kuwezesha timu hii kufanya kazi yao kwa uzuri zaidi.

Habari njema pia ni kuwa, simulations katika tovuti ya PHET huweza kupakuliwa kirahisi na kuweza kutumiwa bila hata ya kuwa na intaneti. Jambo la kufanya ni kupakua "installer" ya simulations hizi, ziweke kwenye kompyuta yako. Hapo utaweza kuzitumia bila ya kuunganishwa na intaneti. 

Tovuti nyingine nzuri ni Absorblearning.com. Tovuti hii ina mkusanyiko wa video, simulations, na picha katika masomo ya Kemia, Fizikia, Hisabati, na Eletronics. Zana za kidigitali katika tovuti hii zinahitaji kulipiwa ili uweze kupakua na kutumia bila intaneti. Uzuri wake ni kuwa, inawezekana kutumia zana hizi ukiwa umeunganishwa na intaneti.

Ukitaka kutumia tovuti hii, chagua somo unalohitaji kwa kuingia kwenye absorb Chemistry, absorb Physics, absorb Mathematics, absorbadvanced physics au absorb Electronics na kisha nenda kwenye linki inayoonesha idadi ya zana zilizopo kwenye somo husika. Kisha tafuta zana kulingana na kile unachokisoma. 

Mtandao wa YouTube pia una video nyingi na nzuri kwa ajili ya walimu na wanafunzi. Tutorvista ni moja ya watumiaji wa YouTube wanaopakia video za kielimu za masomo ya sayansi kwa shule za sekondari. Unaweza kuzipakua vidieo hizo na kuzitumia wakati wowote bila ya kuwa umeunganishwa kwenye intaneti. Kwa ujumla, katika mtandao wa YouTube, kuna video nyingi sana kwa ajili ya wanafunzi kujifunzia na walimu kujitayarisha kufundisha somo. 

Ili kukwepa gharama zaidi za intaneti, ni vyema mwalimu au mwanafunzi akapakua video anazooona zinafaa kuliko kuziangalizia mtandaoni. Moja ya kitumizi kizuri kabisa cha kupakulia video ni internet download Manager (IDM). Kama ni mara yako ya kwanza kuitumia kwenye kompyuta yako, utaweza kuitumia kwa siku 30 na kisha utatakiwa kuinunua.

Baadhi ya tovuti nyingine ambazo unaweza kupata zana za kidigitali za kufundishia na kujifunzia ni pamoja na Math open reference iliyo na mkusanyiko wa animations za jiometri kwa shule za sekondari na learnerstv, yenye mkusanyiko wa zana mbalimbali kwa masomo katika kada mbalimbali za kielimu.

Vyanzo vya zana za kidigitali vinavyofanana na hivi vichache nilivyovizungumzia ni vingi. Jambo la msingi ni kufanya utafiti mtandaoni kulingana na kile ambacho mwalimu au mwanafunzi anakihitaji kwa ajili ya kujisomea au kufundishia.

Pamoja na kuwa kwa sasa, walimu wengi wanamiliki kompyuta, changamoto kubwa hapa ni kuwa, wengi wa walimu wetu hawana mazoea ya kutumia kompyuta na mtandao wa intaneti katika ufundishaji. Katika kituo fulani cha kazi, ilikuwa vigumu sana kuwashawishi walimu kuandaa nukuu, maandalio na maazimio ya kazi kwa kutumia kompyuta. Hali kadhalika kwa wanafunzi, wengi wanatumia kompyuta na simu kwa mambo yasiyo ya kimasomo. Bado tuna kazi pevu ya kuwajengea walimu na wanafunzi utamaduni wa kutmia TEHAMA katika ufundishaji na ujifunzaji.




Comments

Mbele said…
Hii ni mada muhimu. Ni ukweli kwamba maendeleo ya tekinolojia yanatuwezesha kufanya mambo--kama vile kufundisha au kujifunza--kwa namna tofauti na tulivyozoea.

Kila ninapowasikia wa-Tanzania wakisema wanataka wataalam walioko nje warudi nyumbani kusaidia kujenga Taifa huwa najiuliza kama wa-Tanzania wamefunguka mawazo na kutambua kuwa dunia ya leo ni tofauti na ile ya miaka iliyopita.

Kutokana na tekinolojia kama uliyoelezea, mtaalam anaweza kukaa Tokyo au Johannesburg akachangia utaalam wake kwa yeyote duniani.

Mwalimu kama mimi ninaweza kufundisha darasa lenye watu sehemu mbali mbali duniani. Haijalishi uko nchi gani. Mimi mwenyewe ninajibu masuali na kutoa maelekezo kwa watu kutoka sehemu mbali mbali xs dunia, bila kwenda nchini kwao na kuonana nao uso kwa uso.

Wa-Tanzania wajitahidi kuwa na upeo huu.
Albert Kissima said…
Profesa Mbele, shukrani kwa uzoefu wako. Maoni yako ni darasa tosha pia. Watanzania sisi bado ni lile sikio la kufa, lisilosikia dawa. Tunahitaji kubadili sana mitazamo yetu na kuachana na kufanya mambo kwa mazoea.

Kwa ulimwengu wa sasa, ambao mawasiliano yamerahisishwa kupitia tekinolojia, utashangaa kuwakuta walimu wenye simu na kompyuta nzuri pamoja na mtandao wa intaneti wanasubiri serikali iwaletee semina mashuleni.

Kwa mfano, walimu wanasema hawajapata semina za mabadiliko ya mitaala iliyoboreshwa mwaka 2005. Pengine wanazihitaji semina ili wapate posho. Kumbe wangeweza kuendelea kujifunza masuala haya ya mitaala inayoitwa mipya kupitia mitandao ya intaneti. Humo kuna vitabu vingi, majarrida, makala, video n.k

Waalimu tungeweza kuendesha pia mijadala ya kuelekezana masuala haya tukiwa popote Tanzania na duniani. Tungeshafika mbali. Tunasubiri semina mashuleni.
Unknown said…
albert YONA kakuibia hii makala
Albert Kissima said…
Ndio hivyo Mushi. Jamaa alikiuka miiko ya uandishi wa habari. Sawa, aliniomba aiweke kwenye magazeti anayooandikia Mwananchi na Jamhuri ( kama sijakosea). Nilimruhusu, lakini nilijua anafanya hivyo kama namna ya kusambaza maudhui na bila ya kuathiri haki za mwandishi. Bado ninamkumbusha tu kuwa ajitathmini. Sina haja ya kupoteza muda wa kumfuatilia alimradi (angalao) nilichotaka kukifikisha kwa hadhira kilipata wigo zaidi. Ninaimani pia, Yona Maro atajirekebisha.

Popular posts from this blog

Mambo Makuu Manne ya Kuzingatia ili Kufanya Upimaji Endelevu Wenye Tija

Mambo Muhimu ya Kuzingatia Katika Kuboresha na Kuongeza Ufanisi wa Shule.

Kubadilika kwa Mitaala: Walimu na Wanafunzi Wabadilike kwa Namna Gani?