Mambo Makuu Manne ya Kuzingatia ili Kufanya Upimaji Endelevu Wenye Tija



Picha: Blogger.
Upimaji endelevu wa mwanafunzi ndio namna pekee ya kutoa taarifa za maendeleo ya ujifunzaji wa mwanafunzi katika kufikia malengo ya ujifunzaji yaliyokusudiwa kwake. Kwa hiyo, upimaji endelevu ni shuhguli ya msingi mno ya kuzingatiwa na mwalimu na wanafunzi. 

Upimaji endelevu siyo shughuli ya mwalimu peke yake. Ni mchakato wa pamoja kati ya mwalimu na manafunzi. Hii ni kusema kuwa, upimaji endelevu ni sehemu ya ujifunzaji wa mwanafunzi na ufundishaji wa mwalimu. Ikiwa tunahitaji kuona upimaji wenye tija, basi kila mmoja ni lazima atimize wajibu wake kwa kushirikiana.

NWEA katika chapisho lao la mwaka 2016 linaloelezea mambo makuu manne ya kuzingatia ili kuleta ufanisi kwenye upimaji endelevu, wanaeleza kuwa upimaji endelevu  ni mchakato wa pamoja kati ya mwalimu na wanafunzi wa kukusanya ushahidi wa ujifunzaji wa wanafunzi kwa lengo la kuboresha kile kinachoendelea darasani, kwa maana ya mchakato wa ujifunzaji wa wanafunzi.  

Ili kufanya mchakato wa upimaji endelevu kuwa wa mafanikio, wanafunzi wanapaswa kusaidiwa na mwalimju wao kuwa na majibu ya maswali matatu makuu. Kwanza, hadi mwisho wa kipindi, mada au kozi, wanafunzi wanapaswa kuwa wamejifunza nini, wanafunzi wamefikia wapi katika ujifunzaji wao na ni kwa namna gani watakamilisha kile ambacho hawajajifunza ili wafikie malengo yao ya ujifunzaji. 

Maswali hapo juu ni muhimu sana yakaweza kujibiwa na wanafunzi wenyewe kwa kushirikiana na mwalimu wao. Mchakato huu ili uwezekane unahitaji utamaduni mzuri wa kuwajumuisha na kuwashirikisha wanafunzi kwenye upimaji endelevu. 

Hata hivyo, tafiti anuai zinaonesha kuwa kuna ugumu mkubwa wa kuelezea kwa ufasaha namna nzuri zaidi ya kutekeleza  upimaji endelevu wa mwanafunzi (Havover Research, 2014) kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo za upimaji endelevu kuwa na tafsiri tofauti (kulingana na mazingira), aina ya walimu, upatikanaji wa nyenzo za kufundishia na mambo mengine. 

Pamoja na ugumu huu, taasisi ya NWEA inayojihusisha na utafiti wa namna bora za kutekeleza upimaji wa wanafunzi, imebaini mambo makuu manne ya kuzingatia ilikuhakikisha upimaji endelevu unaleta tija kwenye ujifunzaji wa wanafunzi.

 Makala haya yanalenga kujadili mambo hayo makuu manne ambayo ni; ufafanuzi wa kina wa mambo makuu yanayopaswa kujifunzwa na wanafunzi (clarifying learning), kuwajengea wanafunzi ari ya kujifunza (activating learners), kutoa mrejesho wa maendeleo yao (providing feedback) na kutafuta ushahidi wa ujifunzaji (eliciting evidence of learning). 

Ufafanuzi wa Kina wa Mambo Mahususi ya Kujifunza

Ni muhimu sana kwa mwalimu kueleza kinagaubaga mambo mahususi wanayopaswa kujifunza wanafunzi kabla ya kipindi au kabla ya kuanza kufundisha mada. Kwa mujibu wa Hanover Research(2014), kulinganisha kwa ufasaha shughuli za ufundishaji na malengo mahususi ya ujifunzaji yanasaidia kuwafanya wanafunzi wafahamu vizuri umuhimu wa kile wanachojifunza na hivyo kuongeza ari ya ushiriki wao. 

Mitaala inayoandaliwa na kusimawiwa na Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE) ni moja ya mifano hai ya kuigwa sana katika mfumo wetu wa elimu. Ikiwa unapenda kufahamu vizuri zaidi dhana ya umuhimu wa ufafanuzi wa kina wa mambo wanayopaswa kujifunza wanafunzi, basi rejea mitaala ya NACTE. 

Pamoja na ufafanuzi wa kina wa malengo ya ujifunzaji, walimu wanashauriwa pia kuandaa vizuri vigezo vya upimaji ambavyo ni kiongozi cha mwanafunzi kufahamu alipotoka kitaaluma, alipo na anapotakiwa kwenda. 

Katika mitaala yake, NACTE imejitahidi sana kutoa ufafanuzi wa kile mwanafunzi anachopaswa kukijifunza kupitia mfumo wa malengo ya ufundishaji yaliyogawanywa katika sehemu kuu tatu ambazo ni Malengo Makuu (principle learning Outcome(s)), Malengo Wezeshi (Enabling Outcome(s)) na Malengo Wezeshi mahususi(Sub-enabling Outcomes(s)).

Pia, uzuri wa mitaala ya NACTE ni kuwa, malengo wezeshi mahususi yamegawanywa katika shughuli mahususi anazopaswa kuzifanya mwanafunzi ili kuhakikisha anajifunza mambo mahususi yaliyokusudiwa. Sambamba na hilo, kila malengo makuu yana vigezo mahususi vya upimaji kwa ajili ya kusaidia kuonesha viwango vya mafanikio yanayotarajiwa kwa mwanafunzi. 

Hii ni kusema kuwa, mitaala inayoandaliwa vizuri hutoa nafuu na kumrahisishia mwalimu katika kutoa ufafanuzi wa mambo makuu wanayopaswa kujifunza wanafunzi kabla ya ufundishaji. Ni rai yangu kwa wadau wa mitaala kujifunza mfumo wa kuigwa wa mitaala ya NACTE ili kujihakikishia hitaji la kwanza la kutekeleza kwa ufasaha upimaji endelevu wa wanafunzi.  

Kuwajengea Wanafunzi Ari ya Kujifunza

Kama nilivyotangulia kusema, upimaji endelevu ni matokeo ya juhudi za mwalimu na wanafunzi wake. Ni vizuri walimu wakaondoa dhana kuwa, upimaji endelevu ni kutoa jaribio, testi au kazi ya nyumbani tu. Haya ni mambo machache miongoni mwa mambo mengi na muhimu yanayojenga upimaji endelevu wa mwanafunzi. 

Upimaji endelevu ni sehemu ya mchakato wa ujifunzaji wa mwanafunzi. Mwanfunzi anapaswa kujiona kuwa anawajibika kwenye ujifunzaji wake na ni sehemu ya chanzo cha maarifa kwa wanafunzi wenzake. Kufanikiwa kumshawishi mwanafunzi kushiriki kikamilifu kwenye ujfunzaji wake hufanya hata shughuli kama vile testi, majaribio, kazi za nyumbani, majadiliano n.k kuwa na maana kwake na kushiriki kwa lengo la kujifunza.

Zipo tafiti nyingi zinazothitibisha kuongezeka kwa ufaulu wa wanafunzi kunakotokana na kuongezeka kwa ushiriki wao wakati wa ujifunzaji. Moja ya tafiti hizi ni ule uliofanywa mwaka 2014 na Profesa Msaidizi, Daktari Gunuc Selim wa Chuo Kikuu cha Yuzuncu Yil cha nchini Uturuki. Katika utafiti wake uliolenga kutafuta uhusiano ulipo kati ya kiwango cha ushiriki wa wanafunzi kwenye ujifunzaji na kiwango chao cha ufaulu aligundua kuwa ushiriki wa wanafunzi kiakili, kitabia na kihisia kunabashiri ongezeko la ufaulu kwa kiwango cha asilimia 10. 

Utafiti kama huu uliofanywa  nchini Kenya na watafiti Ndiewo, Aloka na Raburu ulenga kufahamu ikiwa mafanikio ya kitaaluma ya wanafunzi wa sekondari nchini humo yalikuwa na mahusiano na kiwango chao cha ushiriki kwenye ujifunzaji. Matokeo ya utafiti yalionesha uhusiano sawia wa ushiriki wa wanafunzi na mafanikio yao kitaaluma. 

Ushiriki wa wanafunzi kikamilifu kwenye ujifunzaji kunaongeza uwezekano wa kupata mafanikio kilelimu kutokana na mambo kadhaa. Wanafunzi hupata nafasi ya kujitathmini-pale walipo, walipotoka na wanapohitaji kwenda-jambo linalowapa hamasa ya kujirekebisha na kuchukua jukumu la kujisimamia kuelekea malengo ya ujifunzaji wao. 

Sambamba na hili, ushiriki wa wanafunzi hutoa fursa ya wanafunzi kufanyiana tathmini, kukosoana na kufundishana. Hii ni kama kusema, kila mwanafunzi anakuwa mwalimu wa mwenzake.Ushiriki wa namna hii unawafanya wanafunzi kuwa wabunifu, kuwa na utayari wa kutatua changamoto wakijua wao ni vyanzo muhimu vya maarifa kwa wanafunzi wenzao na wasingalipenda kuwaangusha. 

Itaendelea…..

Comments

Popular posts from this blog

Mambo Muhimu ya Kuzingatia Katika Kuboresha na Kuongeza Ufanisi wa Shule.

Kubadilika kwa Mitaala: Walimu na Wanafunzi Wabadilike kwa Namna Gani?