Juhudi Binafsi na Ndoto ya Mafanikio: Chachu ya Ufaulu wa Wanafunzi 10 Bora Matokeo ya Kidato cha Nne 2016



                                               Picha na Mwandishi wa Makala haya

Shule nyingi za serikali hususani za kata, zinafahamika kwa kukosa miundombinu rafiki ya kufundishia na kujifunzia.  Katika kutatua changamoto hii, zipo juhudi kadhaa ambazo zimefanyika ikiwa ni pamoja na kuanzisha kampeni ya kuhakikisha kila shule inakuwa na madawati ya kutosha. Hata hivyo, wakati kampeni hii ikiendelea, kuna baadhi ya shule zimeripotiwa kupungukiwa na madarasa ya kujifunzia. 

Kwa upande mwingine, shule zinazomilikiwa na watu binafsi, nyingi zinafahamika kuwa na mazingira bora ya kufundishia na kujifunzia. Sambamba na hilo, shule hizi zimekuwa makini kuhakikisha wanafunzi wanaosajiliwa ni wale wenye uwezo mzuri darasani. Hili huhakikishwa kwa kuwachuja wanafunzi kila wanapomaliza kidato kimoja au muhula. Hii ina maana kuwa, vijana wanaofikia kufanya mtihani wa kidato cha nne au cha pili ni wale waliojihakikishia kufanya vizuri. 

Matokeo ya kidato cha Nne kwa mwaka 2016 yaliyotangazwa Januari 31 mwaka huu, yanaonesha shule binafsi zimefanya vizuri Zaidi kuliko shule za serikali. Kuthibitisha hili, shule 10 bora za kwanza zote zimetoka miongoni mwa shule binafsi. Pia, wanafunzi 10 wa kwanza wametoka katika shule hizi. 

Katika nyakati tofauti, baadhi ya vijana waliofanya vizuri katika mtihani huu walizungumza na kuweka bayana siri ya mafanikio yao. Wengi wetu tunaweza kuishia kusema mafanikio ya shule hizi yanatokana na ukweli kuwa miundo mbinu ya shule hizi ni rafiki pamoja na malipo mazuri kwa walimu. Kuna zaidi ya mambo haya.  Sifa binafsi za mwanafunzi ni miongoni mwa chachu za mafaniko yao. 

Alfred Shauri ni mmoja wa wanafunzi waliopata fursa ya kuweka bayana siri ya mafaniko yake kielimu. Huyu ndiye mwanafunzi (wa shule ya Sekondari ya Feza Boys) aliyefanya vizuri zaidi kuliko wanafunzi wengine wote aliofanya nao mtihani wa kidato cha Nne mwaka 2016.
Shauri anasema, pamoja na miundombinu mizuri ya kujifunzia katika shule yake, juhudi binafsi zimechangia kufikia mafanikio aliyoyapata katika elimu. Akinukuliwa na gazeti la Mwananchi la Februari 1 2017, Shauri alisema;

“Licha ya Feza kuwa shule nzuri na ninayoipenda tangu nikiwa mdogo, lakini hilo halikutosha kunifanya nifaulu, zaidi ya kuweka juhudi na kuamini kuwa ninatakiwa niunge mkono juhudi za walimu  kwa kusoma kwa bidi ili kufaulu”

Mbali na kuelewa kuwa alipaswa kujibidisha katika ujifunzaji, Shauri anaonesha kutambua umuhimu wa kuwa na ndoto ya mafanikio. Aliamini kwa kuweka juhudi atafikia ndoto yake ya kufaulu. Hatimaye ndoto aliyoiishi, ameitimiza kwa kuwa mwanafunzi bora kabisa kwenye matokeo ya Kidato cha Nne 2016. 

Juhudi pamoja na kuwa na ndoto ya mafanikio zimetajwa pia na wanafunzi wenngine kama sehemu ya mambo yaliyochangia kufaulu kwao. Cynthia Mchechu ni mwanafunzi aliyeshika nafasi ya pili kutoka shule ya sekondari ya St Francis ya Mbeya. Mwanafunzi huyu anajivunia kutimiza ndoto yake ya kufaulu vizuri katika masomo yake. Hata hivyo, Cynthia aliweka bayana kuwa, njia pekee ya kufanikisha ndoto yake imekuwa ni kufanyia kazi alichokiamini (ndoto yake ya mafanikio) na hatimaye ikawa kweli. 

Kuwa na ndoto ya kuifikia si jambo geni linapokuja suala la mafanikio. Hii ni mbinu inayotajwa kuwa mhimili na kiini cha mafanikio ya kila anayehitaji kufanikiwa. Mifano ipo mingi sana. kuthibitisha hili, mwandishi wa Kitabu cha "It only Takes A  Minute to Change Your Life" Willie Jolley anasisitiza umuhimu wa kuwa na ndoto ya kuifikia, kuiamini na kuitekeleza. Katika kitabu chake, anatoa mifano ya watu wengi sana waliofanikiwa kuweka ndoto zao na kuzifikia, na sasa wana mafaniko ya kupigiwa mfano.

Uwezo wa kujituma kwa bidii ni tabia inayoongozwa kwa kiasi kikubwa na ndoto ya mafaniko aliyonayo mtu. Kujituma ni kiashiria cha kuikubali ndoto yako, kuiamini na kuifanya kuwa kweli.
Wanafunzi wetu wana ndoto wanazoziamini na wanazohitaji kuzitimiza? Ndoto zao zitatimia kwa kukaa darasani bila kufanya lolote wakimsikiliza mwalimu anavyotoa taarifa ya aliyoyajifunza?Walimu wanawasadia wanafunzi kuwa na ndoto, kuzikubali na kisha kuzifanya kuwa kweli?. 

Dhana ya kujituma kwa bidii kama msingi wa mafanikio haitawezekana kwa wanafunzi walio na mtazamo wa kukaa darasani na kusikiliza mawaidha kutoka kwa mwalimu.  Kwa aina hii ya ujifunzaji, si rahisi kupata wanafunzi wanaoweza kupata ndoto watakazoziamini, kuzikubali na kuzifanya zikawa kweli. 

Tusibaki tunalaumu mazingira magumu ya ufundishaji na ujifunzaji. Ikiwa walimu wanaweza kupata mahali pa kujifunzia na kupata maarifa ya kwenda kuwasilisha darasani, ninaamini inawezekana vyanzo hivi vikasogezwa kwa wanafunzi ili wajitafutie maarifa wao wenyewe chini ya muongozo wa mwalimu wao. 

Akina Shauri na wenzake hawakuridhika na mazingira bora ya shule zao, walitambua umuhimu wa kujituma kukamilisha ndoto zao walizozikubali na kuziamini. Vivyo hivyo, wanafunzi mnaosoma shule za kata, msikatishwe tamaa na mazingira ya shule, weka juhudi, ipate ndoto yako, ikubali, iamini na ifanye iwe kweli kwa kuweka juhudi. 

Kwa mwanafunzi, juhudi ya kwanza kabisa ni kushiriki kikamilifu kwenye ujifunzaji wako. Shiriki kujifunza kwa bidii yale unayopaswa kujifunza. Si utaratibu mzuri kwa mwalimu kujifunza na kisha kuleta darasani yale aliyojifunza na kuyawasilisha kwa wanafunzi. 

Wanafunzi jifunzeni kujifunza. Walimu mna kila wajibu ya kuacha utamaduni wa kuwasilisha yale mnayojifunza kwa wanafunzi. Badala yake, waongozeni wanafunzi wajifunze yale wanayopaswa kujifunza. Tutafute namna tunavyoweza kuwapatia vyonzo vya maarifa mnavyovitumia ninyi kujifunzia. Shukrani kwa ukuaji wa TEHAMA, hii ni moja ya nyenzo muhimu ya kufanikisha hili. 

Tumieni ufundishaji wa Kiudadisi unaomtaka mwanafunzi kujifunza kwa kuweka juhudi ya kupata maarifa kwa kuuliza maswali, kuchunguza, kudadisi, kuwa mbunifu n.k. Hii ni hatua ya awali kabisa ikiwa tuna nia ya dhati ya kuboresha elimu Tanzania. Angalao wanafunzi wabadili fikra zao kuhusu namna wanavyopaswa kujifunza. Uhitaji wa kitu ndio chanzo na chachu ya juhudi ya kukipata kitu hicho. 

Ikiwa tunahitaji wanafunzi wa kaliba ya akina Alfred shauri au Cyntia Mchechu na wengine, basi tuhimize ujifunzaji unaochochea wanafunzi kujituma, kuwa wabunifu na wadadisi. Tuungane pamoja kuhakikisha wawezeshaji wetu wanabadilika na kutumia "INquiry Based Learning Approach" wakati wa kufundishia na kujifunzia.




Comments

Popular posts from this blog

Mambo Makuu Manne ya Kuzingatia ili Kufanya Upimaji Endelevu Wenye Tija

Mambo Muhimu ya Kuzingatia Katika Kuboresha na Kuongeza Ufanisi wa Shule.

Kubadilika kwa Mitaala: Walimu na Wanafunzi Wabadilike kwa Namna Gani?