Uwezo wa Kujiajiri na Kuajirika Una Uhusiano na Namna za Ujifunzaji: Wanafunzi Wanahitaji Ujifunzaji Unaochochea Udadisi.





 Picha Kutoka kwenye Video ya Wanafunzi wa Shule Wildwood IB World Magnet wakitumia mfumo wa ujifunzaji wa Udadisi. Video hii unaweza kuitazama hapa.

Kati mwaka 2005 hadi 2007, Tanzania ilibadili mitaala kutoka kwenye mtazamo wa Mwalimu kama chanzo cha maarifa hadi ile ya Mwanafunzi kama kiichi na chanzo cha ujifunzaji wake. Mabadiliko haya yalihusisha shule za msingi, sekondari na Vyuo vya Ualimu.  

Mabadiliko ya mitaala yalilenga kuandaa wahitimu watakaoweza kukabiliana na soko la ajira, kuweza kujiajiri, kuajirika, kuendana kasi ya mabadiliko ya kiteknolojia, kiuchumi na kijamii ikiwa ni pamoja na kukabiliana na kutatua changamoto zinazokabili jamii zinazowazunguka. Kwa bahati mbaya sana, haijakuwa wazi kama kumekuwa na mabadiliko yoyote ya mitaala kwenye elimu ya Juu. Pengine hali hii inaweza kuchangiwa na ukweli kuwa, mitaala ya vyuo vikuu bado haijaunganishwa pamoja.

Hata hivyo, Tafiti nyingi zilizofanyika nchini Tanzania, zinaonesha kuwa, mitaala hiyo haijaweza kutekelezeka kwa kiwango kilichokusudiwa. Tafiti nyingi zinaonesha kuwa, walimu hawana uelwa wa kutosha wa mitaala hii. Upungufu wa uelewa unaelezwa haswa upo kwenye namna wanavyopaswa kuitafsiri mitaala hii. Changamoto kubwa nyingine ni uhaba wa rasilimali watu na vitu kama vile vitabu vya kutosha, samani na madarasa.

Aina ya ufundishaji unaotumiwa kwa sasa nchini Tanzania, hususani kwa shule nyingi za serikali, ni ule wa mwalimu kufaulisha maarifa kwa wanafunzi. Ujifunzaji ni ule wa kukariri na upimaji wa mwanafunzi ni ule wa kuangalia ni kwa kiasi gani mwanfunzi anakumbuka yale aliyojifunza. Mwanafunzi anapewa nafasi ndogo sana ya kushiriki kwenye ujifunzaji wake mwenyewe. 

Madarasa yamekuwa kama vyumba vya mahubiri. Mwalimu anaingia darasani, anaeleza kile kilichomleta. Akimaliza, anaondoka, anakuja mwalimu mwingine, naye anafanya vivyo hivyo. Wakati wote, wanafunzi wanakuwa wamekaa, wanamsikiliza mwalimu, wanachukua nukuu. Wasipoulizwa maswali, wao ni nadra sana kuuliza. Uzoefu unaonesha, wanafunzi hawapendi hata kuuliza maswali. 

Katika hali hii, ni ukweli usio na shaka kuwa,  mfumo huu haumuandai mwanafunzi kuwa mbunifu, mvumbuzi wala mdadisi. Ni vigumu sana kutegemea mwanafunzi wa aina hii kuleta ushindani unaokusudiwa kwenye soko la ajira, kutatua changamono zake na za jamii, kuendana na mahitaji yanayokuwa kwa kasi ya kiteknolojia na kiuchumi. Tusitegemee kamwe vijana wa aina hii wawe na mtazamo wa kujiajiri na kutengeneza ajira. 

Ni ukweli usiopingika kuwa, leo kuna ajira nyingi sana ambazo ziliandaliwa miaka mingi iliyopita na watu waliojipambanua kuwa ni wabunifu, wadadisi, wanaojituma na wenye uwezo wa kufikiri kwa kina. Chukulia mfano wa mitandao ya kijamii kama vile Twitter na Facebook ilivyoshika kasi miaka ya hivi karibuni. Watu wanaajiriwa kufanya kazi kama wasimamizi wa mitandao hii, watu wanafanya biashara kupitia mitandao, wanajifunza, wanawasiliana kwa urahisi na kwa haraka. Haya yote ni matokeo ya watu wanaojituma. Wanaothubutu wao wenyewe kufanya mambo yaliyo na jita kwao na kwa jamii. 

Wanafunzi wetu tunawaandaa kuwa sehemu ya mabadiliko yatakayoibadilisha Dunia kwa namna chanya? Watu wanaofanikiwa na waliofanikiwa wana tabia ya kujituma bila kukata tamaa. Kama wanafunzi wetu ni wa aina ya kukaa na kuhubiriwa tu, sifa hii muhimu wanafunzi wetu watajifunza lini?

Ni dhahiri kuwa, tunahitaji kuweka kipau mbele kwenye aina ya elimu inayomjengea mwanafunzi utamaduni wa kujibidisha kwenye ujifunzaji wake. Wanafunzi wahame kutoka kwenye mfumo wa ufundishaji unaowafanya kuwa waumini wanaosikiliza mahubiri katika nyumba za ibada. Mfumo unaowafanya wanafunzi kujiona wanahusika moja kwa moja kwenye ujifunzaji wao. Wawaone walimu wao kuwa ni wawezeshaji tu. 

Tunahitaji mfumo unaojenga utamaduni wa kujituma, kujitafutia, kuwa mdadisi, kuvumbua, kuibua mambo mapya na kufikiri kwa kina na kwa tija. Hakuna shaka kabisa kuwa, wanafunzi wa aina hii, wataweza kujiajiri, wataajirika na watatumia maarifa yao vizuri katika mazingira ya kazi na kwenye ulimwengu unaobadilika kwa mambo mengi kila uchao.

Ikiwa tunahitaji kuandaa wanafunzi wanafunzi wa kaliba hii, tunahitaji aina ya ufunsihaji unaofahamika kwa lugha ya Kiingereza kama Inquiry-Based Learning. Sina hakika kama nitakuwa nimetafsiri kwa usahihi wake, ila,  kwa Kiswahili, katika Makala haya, na nyingine zitakazofuata, ninauita mfumo huu kuwa ni  Ujifunzaji wa Kiudadisi.
 
Kuna ushahidi mkubwa wa tafiti unaoonesha kuwa, mfumo huu wa ufundishaji umefaulu kwa asilimia kubwa sana. Kupitia mfumo huu, wanafunzi wanajisikia kuwa sehemu ya ujifunzaji wao wenyewe. Wanapata fursa ya kutatua changamoto hai za jamii wakiwa wanaendelea na masomo yao. Kwa mtazamo huu, wanafunzi wanalewa na kujenga maana pana ya ujifunzaji wao. Hii inakuwa chachu ya kujifunza zaidi na kushiriki kwenye michakato mbalimbali ya ujifunzaji. 

Katika ufundishaji wa aina hii, mwanafunzi hushiriki kutafuta majibu ya kile anachopaswa kujifunza. Majibu hupatikana kwa kufanya utafiti, kuchuguza, kuchambua, kujadiliana na kuwasilisha yale waliyojifunza.  Ujifunzaji huweza kufanyika kwa kusoma vitabu, kutazama video, kutembelea maeneo mbalimbali, kuongea na wataalam husika n.k.

Mwalimu ana wajibu wa kuwapatia wanafunzi maeneo ya ujifunzaji, vifaa na rasilimali nyingine za kuwasaidia wanafunzi kufikia malengo yao kulingana na namna walivyojipanga katika kutatua changamoto inayowakabili.  Mwalimu ana wajibu wa kufanya upimaji na tathmini endelevu ambayo hulenga kufahamu wanafunzi wamefikia wapi, wanakosa nyezo gani na kipi cha kufanya ili kuboresha ujifunzaji wao. 

Katika hali ya kawaida na kwa mazingira yetu ya Tanzania, tunaweza kufikiri kuwa aina hii ya ufundishaji haiwezekani. Tunapozitazama changamoto zilizopo madarasani, kama vile wingi wa wanafunzi na ukosefu wa vifaa vya ufundishaji na ujifunzaji, tunaweza kusema kuwa, ufunsihaji huu hauwezekani, ni mgumu, tusubiri hadi hali itakapotengamaa. 

Mfumo huu unawezekana kabisa. Suala la kwanza ni kubadili mtazamo. Walimu hawana budi kufahamu kuwa, mfumo unaotumika kwa sasa, hauna tija na hivyo kuna ulazima wa kuwafanya wanafunzi wahusike moja kwa moja kwenye ujifunzaji wao. Hata kama mashule yatakuwa kila aina ya nyenzo ya ujifunzaji inayotakiwa, unaweza kushangaa kuwa hata wanafunzi ikawachukua muda kukubali kubadilika. Hii ni kwa sababu ya mazoea na ugumu wa kubadili mtazamo wa namna ya kufanya jambo. Tukiamua tunaweza. 


Katika Makala ijayo, tutaangalia kwa undani Zaidi ni kwa namna walimu wanavyoweza kutumia aina hii ya ufundishaji mashuleni.


Comments

Popular posts from this blog

Mambo Makuu Manne ya Kuzingatia ili Kufanya Upimaji Endelevu Wenye Tija

Mambo Muhimu ya Kuzingatia Katika Kuboresha na Kuongeza Ufanisi wa Shule.

Kubadilika kwa Mitaala: Walimu na Wanafunzi Wabadilike kwa Namna Gani?