Elimu Inayozingatia Uwezo: Bado Inasuasua, Wapi tunakosea?



Picha kwa hisani ya gettingsmart
Elimu inayozingatia uwezo imeshika kasi zaidi kipindi cha hivi karibuni, hususani kwa mataifa ya Ulaya. Nchi kama Marekani imewekeza kiasi kikubwa cha fedha kuhakikisha elimu hii inatumiwa mashuleni na vyuoni ili kuleta ufanisi unaopaswa. Kwa mfano,  blogu ya BlackBoard kwa kushirikiana na Baraza la Elimu la Marekani, tayari wameungana kufanya Tafiti za Elimu Inayozingatia Uwezo.
Utafiti wa hivi karibu wa BlackBoard na Baraza la Elimu la Marekani umejaribu kuangalia ni kwa kiasi gani Elimu Inayozingatia Uwezo inavyoweza kutekelezwa na pia mafuaa yake kijamii na kisera na namna ambavyo mfumo wa krediti na uwezo unavyotafsiriwa na wadau mbalimbali wa elimu.
Kutokana na ukweli kwamba, kiwango cha elimu nchini Tanzania kwa kipindi kirefu kimekuwa kikidorora kadiri siku zilivyokuwa zinaenda, moja ya muarobaini ulionekana ni kuazima mfumo wa Elimu unaozingatia Uwezo.  Hivyo basi, mwaka 2004, Tanzania kupitia Taasisi ya Elimu iliamua kubadili mitaala ya shule za msingi hadi vyuo vya ualimu ili iendane na matakwa ya aina hii ya elimu.
Mtaala uliokuwepo ulionekana umeshindwa kukidhi mahitaji ya sera na mikakati mbali mbali ya kielimu na ya kimaendeleo. Pia, tafiti mbalimbali zilzofanywa na wadau wa elimu ikiwa ni pamoja na Taasisi ya Elimu Tanzania zilionesha umuhimu wa kufanyika kwa mabadiliko ya mitaala ya shule za msingi, sekondari na vyuo vya Ualimu.
Kwa shule za msingi, mitaala inayozingatia ujifunzaji wa kuzingatia uwezo ilianza kutumiaka rasmi mwaka 2006, kwa shule za sekondari na vyuo vya ualimu, mtaala mpya ulianza kutumika rasmi mwaka 2005. Hakuna uhakika kama mabadiliko haya yalihusisha pia vyuo vikuu ambavyo huandaa walimu wa kusimamia utekelezaji wa mitaala mipya mashuleni inayohamashisha ufundishaji na ujifunzaji unaozingatia uwezo.
Hata hivyo, mara baada ya kufanyika mabadili haya ya mitaala, mafanikio katika elimu yameendelea kulegalega kwa kiasi kikubwa. Ni takribani miaka kumi ya utekelezaji wa mitaala inayozingatia Ujifunzaji unaozingatia uwezo. Tumezidi kushuhudia idadi kubwa ya wanafunzi wa shule za msingi wanaomaliza elimu ya msingi bila kujua kusoma, kuandika kuhesabu.
Utafiti wa Twaweza wa mwaka 2012 unaonesha kuwa nchini Tanzania, zaidi ya asilimia 55 ya wanafunzi wa darasa la tatu hawakuweza kusoma hadithi ya Kiswahili ya darasa la pili huku wanafunzi 8 kati ya 10 wa darasa la tatu wakishindwa kusoma hadithi ya kiingereza ya darasa la pili.  Pia, utafiti huo unaonesha kuwa, wanafunzi 7 kati ya 10 wa darasa la tatu hawakuweza kufanya hesabu ya kuzidisha ya darasa la pili.
Elimu ya sekondari nchini Tanzania nayo imekuwa ikisuasua kila kukicha. Matokeo ya mitihani Taifa ya kidato cha nne ya mwaka 2012 ndiyo yaliyokuwa matokeo mabaya katika historia ya mitihani ya Taifa inayosimamiwa na baraza la mitihani la Tanzania ambapo zaidi ya asilimia 65 ya watahiniwa walifeli mtihani huo.
Kufuatia kusuasua huku wa elimu, watafiti na wadau  mbali mbali  wa elimu wamekuwa wakitafiti mfumo huu wa elimu elimu ili kubaini mafanikio, changamoto na kisha kutoa mapendekezo ya nini cha kufanya.
Tafiti nyingi zilizofanyika nchini Tanzania zinaonesha kuwa walimu hawana uelewa wa kutosha kuhusu ufundishaji na ujifunzaji unaozingatia uwezo. Kupitia tafiti hizi, imefahamika kuwa, walimu wengi wa shule za msingi na sekondari hawafahamu nini wanapaswa kutekeleza ili kuhakikisha wanafundisha kwa mujibu wa mitaala ya sasa. Hali kadhalika, tafiti zinaonesha kuwa waalimu wanafunzi wanaotarajiwa kwenda kufundisha mashuleni, hawana uelewa wa kutosha wa kuweza kufundisha kwa kuzingatia matakwa ya ufundishaji unaozingatia uwezo.  Pia, hali isiyoridhisha ya mazingira ya ujifunzaji na ufundishaji inaonekana kuwa ni moja ya mambo yanayopelekea elimu inayozingatia uwezo wa mwanafunzi kuonekana kushindwa.
Wakati tafiti nyingi zinazohusu ufundishaji na ujifunzaji unaozingatia uwezo zikiwa zimeelekezwa zaidi kwa walimu, tuna mswali kadhaa ya kujiuliza.
Kwanza, wahadhiri wa vyuo vikuu wanaufahamu vyema mfumo huu wa ufundishaji na ujifunzaji? Wanapofundisha walimu wanafunzi, fikra zao, ufundishaji wao na maono yao yanasimia kwenye mfumo huu? Vyuo Vikuu nchini Tanzania vinautumia mfumo huu kuwafundisha wanafunzi? Je, vyuo vikuu vinafahamu kwa upana wake misingi ya Elimu Inayozingatia uwezo na inaisimamia ipasavyo kwenye kutoa elimu? Pengine, maswali haya yanapaswa kujibiwa kupitia tafiti.
Hata hivyo, kuna ukweli kuwa,  vyuo vikuu vinatumia zaidi njia ya mihadhara kwenye ufundishaji. Labda wingi wa wanafunzi katika darasa moja inaweza kuwa ni moja ya sababu. Swali la kujiuliza ni kama, ufundishaji wa kuzingatia uwezo unaathiriwa na wingi wa wanafunzi darasani. Kujibu swali hili, ni vizuri kwanza tukaifahamu Elimu inayozingatia ujuzi pamoja na misingi yake. Tukutane katika makala ijayo.

Comments

Popular posts from this blog

Mambo Makuu Manne ya Kuzingatia ili Kufanya Upimaji Endelevu Wenye Tija

Mambo Muhimu ya Kuzingatia Katika Kuboresha na Kuongeza Ufanisi wa Shule.

Kubadilika kwa Mitaala: Walimu na Wanafunzi Wabadilike kwa Namna Gani?