Utaratibu Huu wa Kuoa/Olewa ni Mzuri, Unahitaji Kuboreshwa Kidogo.



Picha kwa hisani ya Gospel Kitaa.
Hakuna asiyejua shughuli ya kuoa/olewa ilivyo na pilika pilika nyingi na za kuchosha.  Siyo tu hupoteza muda na fedha, mara nyingine huishia kwa watu kugombana, kuwekeana chuki na vinyongo visivyoisha.  Asilimia kubwa ya fedha za harusi hutokana na michango ya watu mbalimbali kuanzia ndugu, jamaa na marafiki.
Harusi ni sherehe ifanywayo kwa ajili ya kufurahia tukio muhimu la kufunga ndoa. Sherehe hii huja mara baada ya wapendanao  kufunga ndoa  kanisani, msikitini, serikalini ama kwa utamaduni.  Hadi siku ya ndoa, sherehe ndogo ndogo za awali kama za kutambulishana, yaani ndugu wa pande mbili kufahamiana, kuvishana pete za uchumba, utoaji wa mahari, kapu la mama na send off  hufanyika.
Sherehe ya awali kabisa inayowashirikisha watu nje ya familia ni kapu la mama. Sherehe hii ni sehemu ya maandalizi ya sherehe ya kumuaga msichana (mara nyingi hufanywa upande wa msichana). Hapa mama wa msichana ndiye mhangaikaji mkuu. Hugharamia kiasi cha chakula na vinywaji akitegemea kupata fedha za zaidi za kuandaa sherehe ya kumuaga msichana wake.  Yawezekana utaratibu huu haupo kwa makabila mengine (au upo wa namna kama hii), lakini kwa wachaga, utaratibu huu upo. Baada ya kapu la mama, sherehe inayofuata ni ya send off, ile ya kumuaga mtoto wa kike.
Sherehe ya kumuaga msichana, maarufu kama send off,  imekuwa  moja ya sherehe muhimu katika kuelekea kwenye ndoa. Sherehe hii, huwa na shamra shamra nyingi, wakati mwingine hufana hata kuliko sherehe ya ndoa, yaani harusi. Sherehe hii (mara nyingi) hufanikishwa pia kupitia michango ya ndugu, jamaa na marafiki.
Hata hivyo, kwa sasa hali ni tofauti kidogo. Kuna mfumo mpya unaingia miongoni mwa wanajamii. Ndio unachipukia, lakini nina imani kubwa siku za usoni, utakuwa ni utaratibu. Kama tu wasichana walivyoanza kuvaa hadharani suruali na nguo nyingine za kubana. Mwanzo ulikuwa mgumu, walionekana wasiokuwa na maadili. Kwa sasa, hali ni tofauti, umekuwa ni mfumo wa uvaaji wa kawaida kabisa. Ninaamini, mfumo huu nao utakubalika katika jamii, pamoja na kuwa, unahitaji kuboreshwa (kwa mtazamo wangu).
Kwa hakika sherehe hizi zinagharimu fedha na muda mwingi wa wanajamii. Bahati mbaya, gharama hizi huelekezwa zaidi kwa ndugu, jamaa na marafiki. Michango ya ugonjwa, masomo, ujenzi  n.k haiwezi kupata fedha za kutosha kama ilivyo kwa sherehe hizi za harusi. Hata hivyo ni nadra sana kwa mambo mengine ya kimaendeleo (ya mtu binafsi) na magonjwa kuchangiwa. Watu hawana mpango wa kuchangia mambo ambayo hawatahusika kwenye matumizi ya walichochanga. Hii ni aibu kubwa sana kwa jamii yetu ya kitanzania. Hatuna budi kubadilika.
Kuna wimbi kubwa la vijana wanaopata ridhaa ya kuanza kuishi kama mke na mume mara baada ya kutambulishana. Sherehe ya kutambulishana, mbali na kuwakutanisha ndugu wa pande zote mbili, majirani pia hualikwa katika shughuli hii.  Kwa hiyo, watu wengi hukutana na hivyo sherehe hii huwa kubwa kidogo lakini inayoandaliwa na wanafamilia zaidi. Wakati mwingine, wapendanao hutumia fursa hii kuvishana pete za uchumba. Sherehe hii kwa wanaotarajia kuishi pamoja, huitumia kama tiketi ya kuanza maisha kama wanandoa, hata kabla y kufunga ndoa. Utaratibu huu upo, na ni imani yangu kuwa, siku za hivi karibuni utazoeleka na kuwa utaratibu rasmi.
Kwa mtazamo wangu, mfumo huu unafaa. Ni mfumo nafuu, usiohitaji muda mwingi na kuchangishana fedha kutoka kwa ndugu, jamaa, na marafiki. Bila kujificha kwenye shamba la karanga, mimi ni mmoja wa watu wasiyependa sherehe hizi. Sizipendi kwa kuwa sioni ulazima wake, na pia, wananchi masikini hubebeshwa mzigo mzito wasioumudu. Kwa sasa, kwa mwaka mtu anaweza kuwa na kadi za michango ya harusi zisizopungua tano. Kwa bahati mbaya sana, siku hizi kuna viwango vya kuchanga.Ukichanga chini ya kiasi kilichokubaliwa, adhabu ya kwanza ni kutopewa kadi ya mwaliko.
Watu hawasemi lakini michango hii imekuwa kero kubwa sana kwa wanajamii.  jamii haipendi, wengi hulazimika kuchanga,  msukumo mkubwa ukiwa ni kuchangiwa pindi watakapokuwa na shughuli kama hizo na kutokutengwa katika shughuli za namna hiyo(watu husahau namna wanavyotengwa wakati wa matatizo). Na sababu nyingine ni kuwa, wachangiaji hutegemea kurudisha sehemu ya fedha yao kwa kula na kunywa siku ya sherehe husika. Kununiana na sintofahamu huweza kujitokeza pale mtu aliyechanga fedha yake na hakualikwa kwenye hafla.
 Nimeanza kwa maelezo marefu ili upate picha halisi ya namna shughuli ya ufungaji ndoa inavyoambatana na sherehe  zinazotegemea kufanikishwa kupitia nguvu ya kifedha na muda wa ndugu, jamaa na marafiki.
Mfumo huu wa wapendanao kuanza kuishi mara baada ya kutambulishana, ni mwanzo mzuri wa kuepuka kuitwika jamii gharama zisizo za lazima. Katika mfumo huu (mpya), wapendanao huishi kwa muda, na baadae huja kubariki ndoa kwa gharama nafuu bila ya kuandaa harusi. Pamoja na kuwa watu hawa wanaishi bila kukamilisha ndoa, huu ni mwanzo mzuri wa kupunguza kuitumikisha jamii kwa kuwapotezea muda wao pamoja na kuingia gharama zisizo za lazima.
Ningependa utaratibu huu uboreshwe kidogo. Ndoa ifungwe siku hiyo hiyo ya kutambulishana. Badala ya kuvishana pete ya uchumba, wavishane pete za ndoa kwa kufuata utaratibu wa imani zao. Yaani ndoa ifungwe siku hiyo hiyo ya kutambulishana. Hatua hii ya kuwakutanisha ndugu wa pande mbili, ni ishara kuwa wawili hao, wameshakubaliana kuoana. Taratibu za ndoa zifanyike kama kawaida, ile siku ya kutambulishana, ndoa ifungwe. Mambo yaishie hapo. Huu utakuwa utaratibu nafuu kabisa wa ufungwaji ndoa usiotumia muda mwingi na fedha nyingi za watu.
Natamani vijana wangenielewa. Ninatamani wale wanaotarajia kufunga ndoa wangepanga utaratibu huu. Natamani viongozi wa dini wangeuchukua ushauri huu. Ninafahamu taratibu za kuoa/olewa zinaweza kutofautiana  kulingana na mahali, imani, hata na utamaduni. Lakini, katika hali zote hizi, shughuli hii ni dhahiri kuwa, mfumo wake hugharimu sana fedha na muda wa watanzania.
Vijana sisi ndio wa kuleta mabadiliko, hatuna budi kuyakubali mabadiliko yenye tija, hususani katika zama hizi za ugumu wa ajira. Si sahihi sana kuendelea kushikilia taratibu zisizo na tija, zinazochukua muda na fedha nyingi ambazo zingetusaidia katika shughuli za maendeleo. Ninatambua ni vigumu kuibadili jamii, hususani katika hili, lakini, tukiamua tunaweza.
Nitakuwa mjinga kabisa kama nitapiga vita michango ya kuwasaidia waliopenda kusoma lakini wakakosa fursa hii kwa sababu ya kukosa ada, au kupiga vita mchango wa kumsaidia mtu mgonjwa aliyekosa matibabu bora kwa kukosa fedha ya kugharamia matibabu.
Tumekosa maabara mashuleni, tumekosa nyumba za walimu, tumekosa vyoo vya wanafunzi na walimu, tumekosa fedha ya kuwapa motisha walimu, tumekosa fedha ya kujenga wodi za akina mama wanaolala zaidi ya mmoja katika kitanda kimoja, lakini tunaweza kukusanya mamilioni ya kumwambia mototo wa kike kwa heri, na mamilioni ya harusi ya siku moja.
 Wazazi chonde chonde, tubadilike, huu siyo ustaarabu wala ishara ya ushirikiano. Bila kujali jamii nyingine zinafanyaje, lakini ninapaza sauti yangu kwa jamii ya watanzania, tubadilike. Niungeni mkono, kwa pamoja tuibadili jamii yetu. Tuungane katika mambo ya maendeleo.  Inawezekana wazazi wakakaa na mtoto wao sebuleni, wakampa wosia, wakampa na fedha walizotaka kumuagia kwa send off, aende akaanzie maisha. Ndoa inaweza kufungwa kanisani, msikitini au serikalini na watu wakafurahia siku hiyo majumbani kwao, au kama wanauwezo wa kutosha, wakaalika watu wajumuike nao bila kuwachangisha mamilioni ya shilingi. Mambo haya yanawezekana tukiamua.






Comments

Popular posts from this blog

Mambo Makuu Manne ya Kuzingatia ili Kufanya Upimaji Endelevu Wenye Tija

Mambo Muhimu ya Kuzingatia Katika Kuboresha na Kuongeza Ufanisi wa Shule.

Kubadilika kwa Mitaala: Walimu na Wanafunzi Wabadilike kwa Namna Gani?