Tunawezaje Kuongeza Ufanisi na Ubora wa shule? Watafiti wa Masuala ya Ubora na Ufanisi wa Shule Wanatujuza.
















Wanafunzi wakiwa wamekaa chini darasani huku somo likiendelea katika moja ya shule za msingi mkoani singida. 

Kwa kipindi kirefu sasa, shule za msingi na za sekondari za Tanzania zimekuwa na matokeo yasiyoridhisha.  Kuna idadi kubwa ya watoto wanaomaliza elimu ya msingi pasi kujua kusoma na kuandika. Hali kadhalika, wapo vijana wengi wa sekondari wanaomaliza na kushindwa kupata alama stahiki za kuwawezesha kuendelea na elimu ya juu. Kufuatia hali hii, yapo mengi  yaliyozungumzwa na mikakati kadhaa kufanyika. Miongoni mwa mambo hayo ni pamoja na kuweka utaratibu wa kuandaa walimu wengi wa elimu ya awali kwa shule za msingi. Katika kukabiliana na changamoto za uhaba wa walimu hasa wa sayansi kwa shule za sekondari, mikakati kama ya kutumia teknologia katika ufundishaji na ujifunzaji imeanzishwa.  


Wanafunzi wa shule moja ya msingi mkoani singida wakisomea katika darasa lisilo na ubora kabisa.

Kuhusu ubora wa shule, kuna mambo mengi yamefanyika. Kwanza, kuongeza idadi ya shule za serikali, alimaarufu, shule za kata. Kwa bahati mbaya, shule hizi siku hadi siku zimeendelea kukosa ubora na ufanisi. Mazingira yasiyoridhisha ya kujifunzia na kufundishia imekuwa ni moja ya changamoto kubwa. Changamoto nyingine zimekuwa ni pamoja na kukosekana kwa maabara na maktaba zenye ubora unaotakiwa. Uchakavu wa madarasa na ofisi za walimu imekuwa pia ni sehemu ya changamoto katika shule zetu za msingi na sekondari.
Swali la kujiuliza hapa ni kuwa, katika kukabiliana na changamoto hizi, tunasikiliza na kufuata ushauri wa wataalamu wa tafiti za ubora na ufanisi wa shule au tunafanya lile linalowezekana au kwa kuwa tu wenzetu walipitia huko na wakafanikiwa?
Ubora na ufanisi wa shule ni mambo ambayo kwa kiasi kikubwa yanafanana lakini yana utofauti fulani. Kimsingi, mambo haya yanategemeana na yanakwenda pamoja. Mara nyingi, ni vigumu kuyatofautisha. Ufanisi wa shule maana yake ni nini? Ufanisi wa shule ni utendaji wa shule ambao hupimwa kwa kuangalia matokeo ya shule husika. Matokeo ya shule husika pia hupimwa kwa kuangalia wastani wa mafanikio ya wanafunzi kwa kipindi chote cha ujifunzaji wao. Mafanikio ya mwanafunzi kwa kipindi chote cha mafunzo hupiwa kwa mtihani wa mwisho unaompima mwanafunzi mambo yote aliyojifunza kwa kipindi kilichopangwa. Mitihani ya taifa, ni moja ya njia ya kupima ufanisi wa shule. 
Katika lugha ya kawaida, ninaweza kusema kuwa, ufanisi wa shule hupimwa kwa kuangalia kiwango cha ufaulu wa wanafunzi. Ndio maana hata wazazi hushawishika haraka sana kuwapeleka watoto wao kwenye shule zinazoongoza kwa ufaulu katika mitihani ya taifa. Wakati mwingine, ubora wa shule huwa hauzingatiwi, bali ufanisi wake.
Kwa upande mwingine, ninaposema ubora wa shule nina maana gani? Ubora wa shule ni mjumuisho wa mikakati ya mabadiliko ya kielimu yenye lengo la kuongeza ufanisi wa shule ikiwa ni pamoja na mikakati ya shule kuweza kuendana na mabadiliko husika. Miongoni mwa mabadiliko haya ni pamoja na kuongeza idadi ya madarasa, kuongeza idadi ya walimu na wafanya kazi, kuwaendeleza wafanyakazi n.k Mambo yote haya yanahitaji maandalizi makini ili kuyafanikisha. Shule husika haina budi kujiandaa kikamilifu kupokea mabadiliko haya. Vinginevyo, mikakati itaishia vitabuni tu, utekelezaji utakuwa ni ndoto.

Ufanisi wa shule unaweza kufikiwa kwa namna gani?

Kwa bahati nzuri, hadi sasa, zipo tafiti nyingi zilizokwisha kufanyika zinazohusiana na mambo ya kuzingatia katika kuboresha na kuongeza ufanisi wa shule. Tafiti hizi zimefanyika maeneo mbali mbali ulimwenguni. Watafiti wengi wa tafiti za uboreshaji na ufanisi wa shule wamegundua mambo kadhaa ya msingi ya kuzingatiwa katika kuhakikisha ubora na ufanisi wa shule unafikiwa. 
Watafiti wamegundua kuwa, uongozi (kuanzia ngazi ya serikali hadi mashuleni), ushirikishwaji wa wazazi na jamii, mazingira ya shule, aina ya mwanafunzi na familia atokayo, ubora na wingi wa walimu, njia na mbinu bora za kufundishia, ubora na wingi wa vifaa vya kujifunzia na kufundishia na muda wa mwanafunzi kujifunza, ni baadhi ya mambo ya msingi ya kuzingatia katika kuleta ufanisi wa shule.
Katika makala zitakazofuata, nitajaribu kufafanua, ni kwa namna gani mambo haya, na mengine ambayo hayaja tajwa, yanavyoweza kuchangia ufanisi wa shule. Hata hivyo, mambo haya ya msingi yanayoelezwa na watafiti mbalimbali hayawezi kuleta mabadiliko kama hakuna uwajibikaji.  Binafsi, ninaona uwajibikaji utakaoleta uwajibishwaji ndio msingi wa mambo mengine yote niliyoyataja hapo juu. Kwa maana hii, katika makala zinazofuata, swala hili nalo litajadiliwa kwa kina.

Comments

Popular posts from this blog

Mambo Makuu Manne ya Kuzingatia ili Kufanya Upimaji Endelevu Wenye Tija

Mambo Muhimu ya Kuzingatia Katika Kuboresha na Kuongeza Ufanisi wa Shule.

Kubadilika kwa Mitaala: Walimu na Wanafunzi Wabadilike kwa Namna Gani?